KWA takribani miezi 23 tangu Rais John Magufuli aingie Ikulu, Mapato ya serikali kwa mwezi yameshuka kutoka trilioni 1.4 Desemba 2015 hadi kufikia Sh. 1.2 trilion mwezi uliopita, anaandika Angel Willium.
Mamlaka ya Mapato Tanzania ( TRA), imetoa taarifa ya makusanyo ya mapato kipindi cha robo ya kwanza ya mwaka wa fedha 2017/2018 katika kipindi cha mwezi Julai hadi Septemba 2017.
Katika taarifa hiyo TRA imesema kati ya mwezi Julai hadi Septemba mwaka huu, imekusanya mapato yanayofikia Sh. 3.65 trilioni.
Taarifa hiyo imesema kuwa mwezi Julai TRA ilikusanya Sh. 1.1 trilioni, Agosti Sh. 1.2 trilioni na Septemba Sh. 1.3 trilioni.
Ukigawanya mapato hayo ni kama TRA imekusanya wastani wa Sh. 1.2 trilioni kwa mwezi katika kipindi cha miezi mitatu iliyopita.
Mkurugenzi wa Huduma ya Elimu ya Mlipa Kodi, Richard Kayombo amesema makusanyo hayo ni sawa na ukuaji wa asilimia 1.2 ikilinganishwa na makusanyo ya kipindi kama hicho mwaka wa fedha 2016/2017.
Amesema kuwa kodi za hapa Tanzania zinatokana na viwanda, ajira na kodi za bidhaa zinazotoka nje ya nchi.
“Wananchi wanatakiwa kukagua risiti zao kila wanapopewa ili waweze kuhakiki taarifa zilizoandikwa na kama ni halisi ili kudhibiti wakwepa kodi.
Leave a comment