LAZARO Mambosasa, Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam na Profesa Adelardus Kilagi, Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG) wamefunguliwa mashtaka kwenye Mahakama Kuu ya Tanzania. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) na Watetezi wa Haki za Binadamu (THRDC), ndio waliowafungulia kesi hiyo wakilitaka jeshi la polisi limfikishe mahakamani Tito Magoti, ofisa elimu kwa umma wa LHRC waliomshikilia kwa siku tatu sasa.
Magoti ‘alitekwa’ Ijumaa wiki iliyopita Mwenge, jijini Dar es Salaam lakini baada ya siku moja, Jeshi la Polisi lilieleza kumshikilia bila kueleza sababu na kituo anachoshikiliwa.
Leo tarehe 23 Desemba 2019, Familia ya Magoti, LHRC na THDRC mbele ya wanahabari wameeleza, jana tarehe 22 Desemba 2019 wamefungua kesi kupitia mtandao wakiwashitaki Mambosasa na Kilagi.
Wameeleza, pamoja na kufungua kesi hiyo, wamelaani hatua ya Magoti kushikiliwa na Jeshi la Polisi bila kumfikisha mahakama kama ambavyo taratibu na sheria zinavyoelekeza.
Anna Henga Mkurugenzi Mtendaji LHRC, kwamba jeshi hilo limejenga tabia ya kukamata watu kwa mtindo wa ‘kuteka’ bila kueleza sababu za kukamata watu hao lakini pia kukaa nao kwa muda mrefu.
Pia amelalamikia hatu ya kumnyima ‘mtekwaji’ haki ya kisheria ya kuwa na wakili ikiwa ni pamoja na kusimamia mahojiano kati ya polisi na mtuhumiwa.
Kwa uapnde wa Onesmo Ole Ngurumwa, Mratibu wa THRDC, amesema wamefungua kesi hiyo Jumapili ya tarehe 22 Desemba 2019.
Leave a comment