MAMA Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais, anatarajia kumwakilisha Rais John Magufuli kwenye uzinduzi wa mkutano wa 58 wa Shirika la Mashauriano ya Kisheria ya Nchi za Asia na Afrika (AALCO). Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Hayo amesema Dk. Augustine Mahiga, Waziri wa Katiba na Sheria leo tarehe 19 Oktoba 2019, wakati akizungumza na wanahabari kuhusu mkutano huo unaoafanyika kwa muda wa siku tano, kuanzia tarehe 21 hadi 25 Oktoba mwaka huu, jijini Dar es Salaam.
Dk. Mahiga amesema Mama Samia ataufungua mkutano huo kwa niaba ya Rais Magufuli, siku ya Jumatatu tarehe 21 Oktoba 2019.
“Mgeni rasmi katika mkutano huu atakuwa Mheshimiwa Mama Samia, kwa niaba ya Rais Magufuli,” amesema Dk. Mahiga.
Dk. Mahiga ameeleza kuwa, washiriki wa mkutano huo ni mawaziri wa shera, wanasheria wakuu pamoja na mabalozi wa nchi 48 kutoka barani Asia na Afrika, ambazo ni mwanachama wa AALCO.
“Washiriki ni mawaziri wa sheria na wanasheria wakuu. Na hapa Tanzania utafunguliwa na Makamu wa Rais, Mama Samia,” amesema Dk. Mahiga.
Dk. Mahiga amesema washiriki wa mkutano huo watajadili masuala mbalimbali kuhusu sheria za kimataifa na changamoto zake.
“Umoja huu ulijikita katika sekta ya sheria. Huu mkutano ambao unafanyika kila mwaka, Unajishughulisha na masuala ya kisheria katika jumuiya ya kimataifa. Kuna masuala mengi na changamoto nyingi ambapo nchi moja haiwezi kutatua,” amesema Dk. Mahiga.
Leave a comment