JESHI la polisi nchini limesema kuwa makosa makubwa ya jinai yamepungua kwa asilimia 2.0 ambapo ni sawa na makosa 1,082 kwa kipindi cha Januari hadi Novemba 2019, ambapo yalikuwa 53,685 huku mwaka 2018 yalikuwa makosa 54,867. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Pia ajali za barabarani zimepungua kwa asilimia 26.2 ,ambapo mwaka 2018 majeruhi walikuwa 3,689 na mwaka 2019 majeruhi 2722.
Hayo aliyasema jana jijini Dodoma Msemaji wa Jeshi la Polisi, David Misime wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ambapo alisema kuwa asilimia 75 ya ajali zinasababishwa na uzembe wa binadamu.
“Hii ni hatua kubwa hivyo jeshi la polisi linaendelea kutoa wito kwa wananchi na wadau wote waendelee kutoa ushirikiano kwani swala la ulinzi na usalama ni letu sote,” alisema Misime.
Wakati huo huo, jeshi limejipanga katika kuelekea kipindi cha sikukuu za krismasi na Mwaka mpyakuwa nchi ni shwari na inaendelea kuwa ya amani, utulivu na usalama, nakusema kuwa ushwari huo umetokana na ushirikianao mkubwa ambao jeshi la polisi linaendelea kupata kutoka kwa wananchi na kuwezesha uhalifu wa kijinai na ajali za barabarani kuendelea kupungua.
“Niwafahamishe kwamba jeshi la polisi maeneo yote tumejipanga ipasavyo kuzuia na kupambana na uhalifu na wahalifu katika kipindi hiki, kwani doria za miguu, magari, helikopta, pikipiki, mbwa na farasi katika mikoa na vikosi vyote zimeimarishwa ili kuhakikisha maandalizi na kusherehekea kunafanyika kwa amani,utulivu na usalama,” alisema.
Aidha alisema kuwa kinachotakiwa ni ushirikiano kutoka kwa wananchi hususani katika kuzuia kwani kwa kufanya hivyo kwa pamoja watakuwa wanawanyima wahalifu fursa ya kutenda uhalifu waliokusudia na kusema kuwa wahalifu wanaishi ndani ya jamii kwani anaweza kuwa mwanafamilia, ndugu, rafiki, jirani au mkazi wa eneo moja mnaloishi pamoja.
“Tukishirikiana kupeana elimu juu ya ubaya wa uhalifu,kuchukia uhalifu na kuishi kwa uadilifu tutakuwa tumeshirikiana sote kuzuia uhalifu,” alisema.
Vilevile Misime alisema kuwa jeshi hilo linatoa wito na kusisitiza kila mmoja kutii sheria bila kushurutishwa kwani atakayekiuka wamejiandaa katika nyanja zote kumshughulikia mtu kama huyo kwa mujibu wa sheria,kanuni na taratibu na asiwepo wa kumlaumu.
Hata hivyo aliwataka wamiliki wa maeneo ya sherehe kuzingatia sheria na taratibu walizopewa katika maeneo yao za kuhakikisha usalama unakuwepomjeshi la polisi linataka wageni na wananchi wote wafanye maandalizi na washerekee sikukuu hizo kwa amani, utulivu na usalama.
“Ndiyo maana tumesema tumejiandaa ipasavyo kuwashughulikia wale wachache watakaojaribu kuvunja sheria yoyote iwe inayohusiana na jinai au usalama barabarani”alisema misime.
Pia aliwaonya watu wanaokwepa kusafiri mchana na badala yake kusafiri usiku kwa kudhani kuwa kwa kufanya hivyo wanakwepa mkono wa sheria.
Leave a comment