SERIKALI ya Tanzania, imetenga jumla ya shilingi 200 bilioni kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu kuzunguka Mto Msimbazi, jijini Dar es Salaam. Anaripoti Hamis Mguta … (endelea).
Kauli hiyo imetolewa na Paul Makonda, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam leo tarehe 14 Mei 2019, katika eneo la Jangwani ikiwa ni siku moja baada ya maji kufurika eneo hilo.
Maji hayo yalifurika Jangwani na kusababisha mafuriko huku miundombinu ikiharibiwa ikiwa ni pamoja na magari kuzuiwa kupita.
“Kutokana na adha ambayo imeendelea kujitokeza katika eneo la Jangwani, serikali imetafuta fedha kupitia Benki ya Dunia na pesa iliyotengwa ni zaidi ya Dola Milioni 100.
“Hii ni zaidi ya Bilioni 200, baada ya upembuzi yakinifu kuna uwezekano pesa ikaongezeka au ikapungua kulingana na mahitaji yatakayokuwepo, matumaini yangu jambo hili litakalimika ndani ya muda mfupi,” amesema.
Katika hatua nyingine Makonda amewataka wakazi wa Dar es Salaam kuzingatia usafi, ili kuepuka magojwa ya mlipuko ikiwemo kipindupindu.
“Ninazo taarifa kuna baadhi ya ndugu zetu wameua kurudi kwenye nyumba zao baada ya kuona maji yamekauka, lakini maji wanayotumia kupigia deki ndio hayo yaliyochanganyika na vinyesi na yaliyofunguliwa kutoka kwenye chemba ambayo yanamadhara makubwa zaidi ya kupata magonjwa ya mlipuko pamoja na kipindupindu.
“Wale tuliotoka kwenye maeneo tungesubiri ili hali iwe shwari ili turudi sehemu iliyokuwa salama zaidi,” amesema.
Leave a comment