ALIYEKUWA Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda ameshindwa kura za maoni za Chama Cha Mapinduzi (CCM) Jimbo la Kigamboni jijini Dar es Salaam. Anaripoti Hamis Mguta, Dar es Salaam … (endelea).
Mkutano mkuu wa jimbo hilo umefanyika leo Jumatatu tarehe 20 Julai 2020 katika ukumbi wa Chuo cha Mwalimu Nyerere, Kuvukoni jijini humo ambapo wagombea walikuwa 78.
Mchuano ulikuwa mkali kati ya Makonda aliyeuacha ukuu wa mkoa ili kwenda kuwania ubunge kushinfana na mbunge anayemaliza muda wake, Dk. Faustine Ndugulile.
Akitangaza matokeo, katibu mwenezi wa CCM Mkoa wa Dar es Salaam, Simon Mwakifamba amesema wapiga kura walikuwa 399 na hakuna kura zilizoharibika.
Amesema, Makonda amepata kura 122 huku Dk. Ndugulile akupata kura 190 huku Makonda akipata kura 122.
Temeke
Katika hatua nyingine, Mbunge wa zamani wa Temeke, Abbas Mtemvu amemshinda mbunge wa sasa wa jimbo hilo, Abdallah Mtolea.
Mkutano wa jimbo hilo umefanyikia PTA uliopo viwanja vya Biashara vya Mwalimu Nyerere (Sabasaba) huku msimamizi wa uchaguzi akiwa katibu Mwenezi wa CCM Wilaya ya Kigamboni, Abdallah Pazi.
Akitangaza matokeo hayo, Pazi amesema wapiga kura walikuwa 376 ambapo Mtemvu amepata kura 203, akifuatiwa na Doroth Kilave ambaye amepata kura 182.
Nafasi ya tatu imeshikwa na Makonde Raphael kwa kupata kura 40 huku Mtolea akishika nafasi ya nne kwa kupata kura 22.
Itakumbukwa, Mtolea alikuwa mbunge wa jimbo hilo kupitia Chama Cha Wananchi (CUF) katika Uchaguzi Mkuu wa Tarehe 25 Oktoba 2015 lakini ilipofika tarehe 15 Novemba 2018 alijizulu ndani ya Bunge na kuhamia CCM.
CCM ilimpitisha tena kuwania ubunge wa jimbo hilo na kushinda.
Misungwi
Katika jimbo la Msungwi jijini Mwanza, aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Alexander Mnyeti ametangazwa kuongoza kura hizo za maoni na Msimamizi wa uchaguzi, Jamal Babu kwa kupata kura 406 dhidi ya 259 za mbunge anayemaliza muda wake, Charles Kitwanga.
Iringa
Jimbo la Iringa Mjini, aliyekuwa mwenyekiti wa CCM mkoa huo, Jesca Msambatavangu amepata kura 190, nafasi ya pili Nguvu Chengula kura 75 na Ibrahimu Ngwada akipata kura 44.
Katika Jimbo la Mufindi Kusini, David Kihonzile ameongoza kwa kura 216, Dickson Lutevele kura 162 na Josephat Mwagala akipata kura 160.
Arumeru
Aliyekuwa mbunge wa Arumeru Mashariki kupitia Chadema, Joshua Nassari ameangukia pua katika kura za maoni jimbo hilo ndani ya CCM kwa kushika nafasi ya nne akipata kura 23.
Aliyeibuka mshindi kwenye kura hizo ni mbunge wa sasa anayemaliza muda wake, Dk. John Pallagyo aliyepata kura 536 akifuatiliwa Dan Pallagyo kura 63.
Siha
Naibu waziri wa afya, Dk.Godwin Mollel ameongoza kura za maoni Jimbo la Siha Mkoa wa Kilimanjaro kwa kupata kura 148 akifuatiwa na Mkuu wa Mkoa wa zamani wa Tabora, Agrey Mwanry kura 147. Nafasi ya tatu ameshikwa na Tumsifu Kweka kura 53.
Arusha Mjini
Aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo ameibuka mshindi wa kura za maoni za jimbo la Arusha Mjini kwa kupata kura 333 akifuatiwa na Philemon Mollel kura 68 na wakili Albert Msando akipata kura 19.
Endelea kufuatilia MwanaHALISI Online na MwanaHALISI TV kwa habari zaidi
Leave a comment