WAZIRI Mkuu wa Jamhuri ya Muungano Tanzania, Kasimu Majaliwa, amewataka viongozi na waumini wa dini ya Kiislamu nchini kuacha kugombania vyeo na misikiti badala yake waimalishe umoja, amani na mshikamano ndani ya dini ya Uisamu. Anaripoti Dany Tibason … (endelea).
Majaliwa alitoa kauli hiyo leo wakati alipokuwa akifungua Mkutano Mkuu wa kikatiba wa Baraza la Waislamu Tanzania (Bakwata) uliofanyika mjini Dodoma.
Amesema kuwa ni wakati wa viongozi pamoja na waumini wa dini ya kiislamu kukaa pamoja na kujipanga katika kufanya masuala ya kimaendeleo badala ya kutumia muda mwingi kugombania vyeo na umiliki wa misikiti jambo ambalo alisema aliufanyi uislamu kuwa na afya.
Katika hotuba yake ya ufunguzi wa mkutano huo, amesema kuwa pia viongozi wa dini hiyo kwa kushirikiana na viongozi wa dini nyingine wanatakiwa kukemea baadhi ya viongozi ambao wamekuwa wakifisadi mali ya Umma au mali za dini.
Amesema jukumu kubwa la viongozi wa kidini ni kuhakikisha wanawafundisha waumini wao kuwa na hofu ya kimungu ili kufanya kazi bila kufisadi mali za Umma au mali za dini zao na badala yake wawe na uzalendo wa nchi na mali zao.
Katika hatua nyingine Majaliwa aliitaka Bakwata kuhakikisha inahakiki mali zake zote ili ziweze kutumika kwa malengo yaliyokusudiwa na si vinginevyo.
Kwa upande wake Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, na Serikali za Mitaa (Tamisemi) Suleiman Jafo, amewata viongozi wa dini hiyo kuhakikisha wanasaidia serikali pamoja na wananchi kwa ujumla kwa kufanya shughuli za kimaendeleo.
Jafo amesema ni wakati sahihi kwa dini ya kiislamu kuwekeza katika masuala mazima ya kimaendeleo ikiwa ni pamoja na sekta ya Afya, elimu na kiuchumi.
“Kutokana na serikali kujikita katika kutoa huduma mbalimbali kwa wananchi wote, ni wajibu sasa wa viongozi wa dini kuwaimiza waumini wao kutunza miundombinu ya barabara, rasilimali fedha pamoja na kulinda umoja wa dini zote za kiislamu,” amesema Jafo.
Naye Mufti Mkuu wa Tanzania, Sheikh Abubakar Zubeir Ali amesema kwa sasa wamejaribu kuirudisha Bakwata kwa waumini wa dini ya kiislamu tofauti na ilivyokuwa hapo awali kwa maana ya kuwa mbali na waumini wa dini hiyo.
Amesema kwake ni mara ya kwanza kufanyika kwa mkutano mkuu wa Bakwata ambao ni mkutano wa kikatiba na hiyo inatokana na kuwepo kwa changamoto mbalimbali ambazo zilikuwepo.
Mufti amesema licha ya kuwepo kwa changamoto ya kifedha lakini baraza liionekana kuwa mbali na waumini wa dini hiyo jambo ambalo lilimewafanya viongozi pamoja na waumini kutokuwa tayari katika mambo mbalimbali ya kimaendeleo.
Akizungumzia kuhusu mali za Bakwata amesema kuwa kwa sasa baraza hilo linaendelea kufuatilia mali zake na kuzirejesha huku wakiendelea kutatua migogoro mbalimbali ya ndani na kuendelea kujienga mahusiano mazuri katika dini zote ndani ya uisilamu pamoja na mahusiano mazuri kwa nchi rafiki ya Morocco.
“Mwelekeo wa Bakwata katika siku za usoni ni kufanya kila linalowezekana ili kuongeza imani ya waislamu kwa Bakwata na viongozi wake kwa ngazi zote, kukuza uwezo wa Baraza kutoa huduma za afya, elimu ya dini na sekula kwa kutengeneza mtandao mpana wa mashule, vyuo vya ufundi na vyuo vikuu.
“Kuongeza uhusiano mwema na nchi na taasisi za kitaifa na kimataifa ili tusaidiane nao kukuza uwezo wa kiuchumi na kitaaluma, kujenga uwezo wa kudumu kiichumi ili kuiwezesha Bakwata kukidhi mahitaji ya wafanya kazi na waislamu kwa ujumla, kujenga tawi la chuo kikuu cha Al azhar shariif kwa kushirikiana na taasisi ya Alaz har Sharif ya nchini misri pamoja na kusambaza mtandao wa vyuo vya Darul maarif kila mkoa na wilaya nchi nzima,” amesema Mufti Mkuu.
Leave a comment