VIONGOZI mbalimbali wa kisiasa pamoja na watu mashuhuri hapa nchini akiwemo Rais John Magufuli, wametoa salamu za kuwatakiwa heri wanawake katika kilele cha maadhimisho ya siku ya Wanawake Duniani, anaandika Pendo Omary.
Itakumbukwa kuwa maadhimisho ya kiserikali ya siku ya wanawake duniani, yanayofanyika hapa nchini yamebeba kauli mbiu inayosema, “Tanzania ya wiwanda: Wanawake ni msingi wa mabadiliko ya kiuchumi.”
Kauli za baadhi ya viongozi kuhusu siku hii;
Rais John Magufuli
“Nachukua nafasi hii kuwapongeza wanawake wote katika kusherehekea siku ya wanawake duniani. Aidha ninawapongeza wanawake wa Tanzania kwa kuendelea kuunga mkono juhudi za serikali katika maendeleo. Mungu awabariki wanawake wote.”
Ummy Mwalimu- Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
“Tuwekeze kwenye Elimu ya Wasichana. Hii ndiyo njia bora ya kuhakikisha wanawake wanashiriki kikamilifu kwenye ujenzi wa Tanzania ya viwanda. wekeza kwenye elimu ya msichana. Inalipa!”
Zitto Kabwe, Mbunge wa Kigoma Mjini
“Nimeshiriki siku ya wanawake duniani kwa kuandikisha kwenye Hifadhi ya Jamii (NSSF), vikundi vya wanawake wa kata za Buzebazeba na Machinjioni, Manispaa ya Kigoma Ujiji. Kwa mwaka huu wa fedha 2016/17 jumla ya wanawake 210 kutoka kata 7 wataandikishwa kwenye hifadhi ya Jamii kupitia mfuko wa NSSF.
“Kupitia mfuko wa Maendeleo ya Jimbo (CDCF) wanawake hawa watachangia asilimia 50 tu ya michango inayotakiwa, na asilimia 50 nyengine itachangiwa na mfuko wa maendeleo ya jimbo.”
Mwigulu Nchemba- Waziri wa Mambo ya Ndani
“Heri ya siku ya wanawake, mwanamke ni nembo ya familia. Utu, ujasiri, bidii, uaminifu na umoja. Najivunia uwepo wenu.”
Edda Sanga – Mkurugenzi Mtendaji Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake (TAMWA).
“Tulikotoka ni mbali na hakika tumepiga hatua kubwa, wanawake wameanza kuonekana kwenye kila sekta ikilinganishwa na wakati harakati hizi zinaanza.”
Leave a comment