RAIS John Magufuli ametangaza kumteua Profesa Palamagamba Kabudi, na Abdallah Bulembo, Mwenyekiti wa Jumuiya ya wazazi ya Chama Cha Mapinduzi kuwa wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano, anaandika Charles William.
Prof. Kabudi ni mhadhiri katika Kitivo cha Sheria, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Katibu wa Baraza la chuo hicho. Anakumbukwa na wengi kutokana na umahiri wa kujenga hoja aliouonesha wakati akiwa mjumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, maarufu kama tume ya Jaji Warioba.
Taarifa iliyotolewa leo na Gerson Msigwa, Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu imesema kuwa, wabunge hao wawili wanatarajia kuapishwa hivi karibuni kulingana na utaratibu wa Bunge.
Uteuzi wa Prof. Kabudi na Bulembo umezua mijadala mbalimbali huku minong’ono ya mabadiliko ya Baraza la Mawaziri ikianza kusikika, hasa uteuzi wa Prof. Kabudi ukidhaniwa kwamba huenda ikawa ni hatua moja mbele kabla ya kumteua kuwa waziri.
Bulembo anakumbukwa zaidi kwa kazi kubwa ya kusimamia kampeni za Rais Magufuli katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015 ambapo ndiye aliyekuwa mkuu wa msafara wa kampeni hizo, akizunguka karibu nchi nzima pamoja na aliyekuwa mgombea wa CCM.
Bulembo alishatangaza kutomuendelea na siasa za ndani za CCM kwa maana ya kugombea katika uchaguzi mkuu wa chama hicho utakaofanyika mwaka huu na hivyo uteuzi wa Rais Magufuli unaashiria kuendelea kumbakiza mwanasiasa huyo katika medani ya siasa kupitia Bunge.
Leave a comment