JOHN Magufuli, Rais wa Tanzania amevijia juu vyombo vya habari vinavyowataja na kuwahusisha marais wastaafu Benjamin Mkapa na Jakaya Kikwete kwenye ripoti ya mikabata ya madini ya michanga wa dhahabu (Maknikia), anaandika Hamisi Mguta.
Ameyasema hayo leo kupitia taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu, Gerson Msigwa muda mchache baada ya kufanya mazungumzo na Prof. John Thornton, Mwenyekiti wa Barrick Gold Corporation ambayo ni mmiliki mkubwa wa kampuni ya ACACIA Mining Limited.
“Nimesoma ripoti zote mbili hakuna mahali ambapo Mzee Mkapa na Kikwete wametajwa, vyombo vya habari viache kuwachafua hawa wazee, walifanya kazi kubwa kulitumikia taifa letu, viwaache wapunzike,” amesema rais Magufuli.
Baada ya kutolewa kwa ripoti hiyo ya pili, Marais hao wastaafu wamekuwa wakihusishwa kwenye sakata hilo la madini hasa kusainiwa kwa mikataba hiyo ya madini.
Marais hao wastaafu pia wametajwa bungeni kwa madai kuwa hawawezi kuwa salama katika sakata hilo kwani haiwezekani mawaziri wakuu wapitishe bila ya idhini ya viongozi wao wakuu.
Hata hivyo, Rais Magufuli amesema katika mazungumzo yake na Prof. Thornton amesema kampuni yake ipo tayari kufanya mazungumzo na Tanzania yatakayozingatia maslahi ya pande zote mbili na ipo tayari kulipa fedha zote ambazo inapaswa kulipa kwa Tanzania.
Katika taarifa nyingine, Harrison Mwakyembe, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo amesema baada ya rais kupokea ripoti ya mchanga wa dhahabu baadhi ya vyombo vya habari vimechukua fursa hiyo kurusha kila aina ya tuhuma kwa marais wastaafu.
“Ikumbukwe kwamba taarifa iliyotolewa na Kamati haikuwataja wala kuwatuhumu marais hao wastaafu, naviasa vyombo vya habari na mitandao ya kijamii kuacha mara moja muelekeo huo hasi ambao unakila dalili ya kupotosha kampeni tuliyonayo ya kujikomboa kiuchumi,” amesema Mwakyembe.
Hiyo mikataba ilisainiwa na nani aliyekuwa na imaya ya nchi