MADIWANI wa Halmashauri ya wilaya ya Chamwino, Dodoma wamemuomba Mkurugenzi Mtendaji wa halmashauri hiyo, Athumani Masasi, kuwachukulia hatua za kinidhamu watumishi wanaoibia mapato ya ushuru wa mazao waliopo kwenye vizuizi vilivyopo vijijini. Anaripoti Danson Kaijage, Chamwino … (endelea).
Kauli hiyo imetolewa kwa pamoja na madiwani hao wakati walipokuwa wakichangia kwenye kikao cha baraza la madiwani cha kujadili taarifa za utekeleaji za kamati za kudumu zilizotolewa na wenyeviti kilichofanyika Chamwino.
Akizungumza kwa niaba ya madiwani wengine Mwenyekiti wa Kamati ya Fedha, Uongozi na Mipango, Samwel Kaweya alisema kuwa baadhi ya watumishi waliopewa dhamana ya kukusanya ushuru wa mazao siyo waaminifu na hawana uchungu wa halmashauri hiyo.
“Hivyo tunakuomba Mkurugenzi wetu kuwa macho kwa watumishi hao wanaofanya kazi kwenye vizuizi ambao walipewa dhamana ya kukusanya ushuru,baadhi yao siyo waaminifu kwa upande wa fedha pia wanatuangusha hawa,” alisema.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Chamwino, Athumani Masasi amewataka watumishi wake kusimamia kwa uaminifu na ueledi katika ukusanyaji wa vyanzo vya mapato kwa vitendo. Ili kuiongezea halmashauri mapato ya kutosha.
Alisema ili kuvuka malengo ya ukusanyaji wa mapato hayo watendaji waliopewa dhamana wakasimamia kwa uaminifu vyanzo vyote vinavyoiingizia halmashauri mapato ikiwa kwenye ushuru wa mazao.
“Madiwani na watendaji inatubidi kuongeza kasi katika ukusanyaji wote wa vyanzo vya mapato, li tuweze kufikia malengo ya juu zaidi, hii inawezekana pale ambapo kila mtumishi atasimama kwenye sehemu yake kwa uaminifu pia watakuwa wakimuunga mkono juhudi zake Rais John Magufuli katika mpango wake uchumi wa viwanda vya kati,” alisema.
Katika kikao hicho kamati mbalimbali zilipitisha bajeti zake za robo mwaka wa pili ya 2018/19 Oktoba hadi Desemba ikiwemo ya fedha na mipango, ambayo ilikusanya jumla ya Sh. 16,705,663,412 kutoka kwenye vyanzo vyake vya mapato ambayo ni sawa na asilimia 43 ya makisio ya mwaka wa fedha.
Huku kamati zingine zikichangia mamilioni ya fedha kwa ajili ya utekelezaji wa shughuli mbalimbali za miradi ya maendeleo kwa ajili ya Halmashauri hiyo ya Chamwino.
Leave a comment