WAFANYABIASHARA ndogondogo ‘Machinga’ wa kata tatu Kingo, Sabasaba na Chamwino, Morogoro wamepokea misaada ya vitu mbalimbali vyenye thamani ya Sh. 3 milioni kutoka kwa Taasisi ya Kuhudumia Wakimbizi ya Tanganyika (TCRS), ili kuwasaidia kukua kiuchumi na kufikia uchumi wa kati. Anaripoti Christina Haule, Morogoro … (endelea).
Vifaa vilivyotolewa ni pamoja na meza, viti na masufuria, vifaa vya saloon za kike na kiume, pampu za umwagiliaji, vifaa vya kutengenezea mabatiki, cherehani, pamoja na masanduku ya kuhifadhia kukumbukumbu na fedha za vyama vya kuweka na kukopeshana (VICOBA) vyote kwa pamoja vikiwa na thamani ya shilingi milioni tatu.
Mwenyekiti wa kikundi cha Upendo katika kata ya Sabasaba, Tatu Kavula, alisema wao kama kikundi cha wajasiriamali wadogo, wamepokea vifaa hivyo wakiwa na furaha na matumaini makubwa na kwamba watavitumia vizuri ili viweze kuwasaidia kujikwamua kiuchumi wao kama kikundi, familia zao na Taifa kwa ujumla.
Naye Diwani wa kata ya Sabasaba, Mudhihiri Shoo, alisema misaada iliyotolewa kwa kikundi hicho cha Upendo ipo katika mikono salama na kwamba watahakikisha wanawafuatilia kwa karibu wanakikundi hao ili waweze kuendeleza kikundi hicho ambapo alisihi wanakikundi kuvitumia vifaa hivyo kwa manufaa ya kikundi na kuhakikisha kuwa wanaimarisha umoja wao ili waweze kujikwamua kiuchumi na kufikia uchumi wa kati.
Akikabidhi misaada hiyo Msimamizi wa Mradi wa Taasisi ya TCRS mkoa wa Morogoro, Rehema Samuel, alisema wameamua kuwaunganisha wajasiliamali wadogo katika vikundi ili kuunganisha nguvu ya pamoja na kwamba hiyo ni njia rahisi itakayowafanya wapate usaidizi wa haraka ikiwa ni pamoja na kukopesheka katika taasisi za kifedha na kuendeleza biashara zao.
Leave a comment