Tuesday , 19 March 2024
Home Habari Mchanganyiko Machinga Makoroboi Mwanza walia na viongozi kuuza maeneo
Habari Mchanganyiko

Machinga Makoroboi Mwanza walia na viongozi kuuza maeneo

Soko la Makoroboi Mwanza
Spread the love

WAFANYABIASHARA ndogo ndogo (machinga) katika soko maarufu la Makoroboi jijini Mwanza, wanaulalamikia uongozi wa Muungano wa Machinga Tanzania (Shiuma) kutokana na vitendo vyao vya kuuza maeneo ya machinga kwa mabavu kinyume na utaratibu. Anaripoti Moses Mseti, Mwanza … (endelea).

Wamesema machinga wengi katika eneo la Makoroboi na maeneo mengine jijini hapa, wamekuwa wakitozwa pesa kuanzia Sh. 600,000 na kuendelea ili kupatiwa eneo la kufanyia shughuli zao.

Baadhi ya machinga hao wakizungumza katika kikao cha pamoja kilichofanyika eneo la Makoroboi, walisema viongozi hao pamoja na mwenyekiti wa muungano huo kwa kipindi kirefu wamekuwa wakitumia nafasi zao kuwakandamiza ikiwemo kuwanyang’anya maeneo yao kwa mabavu.

Magdalena Daniel ambaye ni msusi katika eneo hilo, alisema mwenyekiti huyo na viongozi wenzake walimtoa eneo lake ambalo alikuwa akifanyia shughuli zake na kuliuza kwa mtu mwingine kwa Sh. 600,000.

Alisema tarehe 8 Agosti, 2018, mwenyekiti huyo (Ernest Matondo) na viongozi wenzake walichukua eneo lake pamoja na thamani mbalimbali za saluni yake ikiwemo viti na kioo kikubwa cha saluni pamoja na kufikishwa polisi na kubambikizwa kesi ya jinai.

“Hawa viongozi wamekuwa na tabia ambayo sio ya kiungwana, wameanzisha utaratibu wa kunyang’anya watu maeneo yao na ukionekana kupinga na kuuliza kitendo hicho wanakupeleka Polisi na kukusingizia kesi.

“Sisi kama machinga Makoroboi tumewachoka kwa vitendo hivyo, haiwezekani wanachukua vitu vyetu kwa nguvu kisa uongozi wao ambao wanaufanyia makoroboi tu lakini hatuoni wanaenda mikoa mingine wao kwanini wanazunguka hapa tu,” alisema Magdalena.

Naye Michael Chacha, alisema machinga wanaofanya shughuli zao katika eneo hilo, hawawatambui viongozi hao wanaochukua maeneo yao kwa nguvu na kuyauza kwa watu wengine wanaokwenda kutafuta maeneo ya kufanyia biashara na kwamba tayari walishawakataa.

Alisema eneo la Makoroboi linalotumiwa na machinga hao lilitolewa na serikali (jiji) bure lakini wanashangazwa kuona viongozi hao wakiuza eneo ambalo limetolewa bure huku akidai kuwa viongozi hao akiwemo Matondo sio machinga na wala hawana eneo la biashara.

“Hatujawai kuona viongozi wa aina hii ndugu zangu eneo ni la bure tumepewa lakini wao wanautaratibu hakuna machinga ambaye ataingia Makoroboi bila kutoa hela na pesa inatolewa kulingana na mtu atakavyoenda na wengine wanatoa mpaka shilingi milioni mbili,” alisema Chacha.

Kwa upande wake aliyekuwa mlezi wa machinga hao, Alfred Wambura alisema vitendo hivyo alishawahi kuvisikia kwa wafanyabiashara hao huku akisisitiza kwamba viongozi hao michezo hiyo wameizoea na siyo jambo la uongo.

Alisema kuwa viongozi hao wanaotuhumiwa hususani mwenyekiti huyo, wamekuwa wakifanya kwa watu wengi na kwamba hata yeye wameanzisha vuguvugu la kutaka kuchukua eneo lake ambalo anafanyia shughuli zake kwa miaka 20 sasa.

“Shiuma sasa limebaki kundi la kutengeneza migogoro, hivi karibuni wameenda kwa Katibu Mkuu wa CCM (Bashiru Ally) kuongea uongo kwamba nimehodhi eneo lote la Makoroboi na hiyo yote wanataka wapewe waanze kuuza.

“Mimi nilikuwa mlezi wao kwa sababu ni miongoni mwa viongozi ambao tulianzisha muungano huu kwa ajili ya kuwasaidia machinga wa hapa Makoroboi lakini tuliamua kujiondoa kutokana na vitendo hivyo vya kuuza maeneo ya watu hovyo,” alisema Wambura.

Alisema eneo hilo ambalo lipo Makoroboi, yeye anaendesha shughuli zake kisheria na vielelezo vyote ninavyo vya kumiliki hapa, na kwamba yeye kwa sasa anawaangalia tu wanavyosumbuka kupeleka majungu kwa viongozi.

Mwenyekiti wa Muungano wa Machinga (Shiuma), Ernest Matondo, alipotafutwa kuzungumzia suala hilo, alisema tuhuma zote anazotuhumiwa siyo kweli na kwamba tayari Taasisi ya kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) walishachunguza.

“Hizo tuhuma kuna dada mmoja alishaenda Takukuru kupeleka hizo taarifa kwamba tunauza maeneo yao lakini TAKUKURU walipochunguza walibaini ni uongo hakuna kitu kama hicho kwa hiyo hizo sio taarifa za kweli,” alisema Matondo.

Matondo alisema kuwa tuhuma dhidi yake pamoja na viongozi wenzake zinatolewa kutokana na wao (uongozi) kuanza kudai eneo la wazi la Makoroboi ambalo linamilikiwa na Alfred Wambura huku akisisitiza kwamba eneo hilo ni lazima walichukue kwa sababu ni la serikali.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari Mchanganyiko

Diwani, wananchi wengine 463 wahama Ngorongoro

Spread the loveMakamu mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Ngorongoro ambaye pia...

ElimuHabari Mchanganyiko

GGML yawapa mbinu wanafunzi Geita Boys kufikia malengo ya kitaaluma

Spread the loveKampuni ya Geita Gold Mining Limited (GGML) imetoa mafunzo maalumu...

Habari MchanganyikoKimataifa

Shule zafungwa kutokana na ongezeko la joto

Spread the loveSUDAN Kusini imeamuru kufungwa kwa shule zote kuanzia leo Jumatatu,...

Habari Mchanganyiko

Bunge laja na Marathon kuchangia ujenzi wa sekondari

Spread the loveBUNGE la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania linatarajia kukusanya fedha...

error: Content is protected !!