MAALIM Seif Sharif Hamad, Mshauri Mkuu wa Chama cha ACT-Wazalendo, amewataka wanachama na viongozi wa chama hicho kuwa macho. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Akizungumza na wanahabari katika Ofisi Kuu ya chama hicho visiwani Zanzibar tarehe 2 Desemba 2019, mkongwe huyo wa siasa za upinzani ametuhumu Chama Cha Mapinduzi (CCM), kupanga mikakati ya uvamizi dhidi ya majengo ya chama hicho sambamba na kuvuruga amani.
“Kuna njama za kihalifu zenye lengo la kuvuruga amani na utulivu nchini, kwa kuvamia majengo mbalimbali yanayotumika kama ofisi za chama (ACT-Wazalendo) visiwani Unguja na Pemba,” amesema Maalim Seif.
Amedai, mpango huo wa vurugu ulitarajiwa kuanza Jumapili, tarehe 1 Desemba 2019, Pemba na baadaye maeneo mengine ya visiwa hivyo.
Ametuhumu Chama cha Wananchi (CUF), kushirikiana na CCM katika kukamilisha mpango huo uliolenga kuwakamata viongozi wa ACT-Wazalendo.
“Baada ya kupangwa, jana Pemba kulifanyika majaribio kadhaa ya kutekeleza mpango huo ovu na uliokusudiwa kuleta shari na kuvunja Amani,” amesema na kuongeza;
“…katika kutekeleza njama hizo, waliwaingizwa katika gari na kuzungushwa katika maeneo ya Mkoa wa Kusini Pemba yakiwemo Mkoani, Mtambile, Kangani na Chake Chake wakijaribu kutaka kutekeleza kazi waliotumwa. Bahati nzuri waliwakuta wenyeji wako vizuri, na wakiwa tayari kwa lolote na hivyo kushindwa kutekeleza uovu wao huo.”
Miongoni mwa mambo anayotaja Maalim Seif kama mpango wa kuvuruga amani, ni pamoja na kuondolewa bendera za ACT-Wazalendo kwenye ofisi zao.
“Tukio la kwanza la upachuaji wa bendera ya ACT – Wazalendo lilifanywa siku ya Jumatano, tarehe 27 Novemba 2019 majira ya saa 6:00 mchana kwenye Ofisi ya Tawi la Bandamaji, Jimbo la Chaani, Mkoa wa Kaskazini Unguja.
“Tukio jengine la upachuaji wa bendera ya ACT – Wazalendo lilifanywa siku ya Ijumaa, tarehe 29 Novemba 2019 majira ya saa 5:00 asubuhi kwenye Ofisi ya Tawi la Mbuyuni, Michamvi, Jimbo la Paje, Mkoa wa Kusini Unguja. Matukio haya yameripotiwa polisi lakini hakuna hatua zilizochukuliwa hadi sasa,” amesema Maalim Seif.
Kutokana na dalili hizo, Maalim Seifa ambaye alikuwa Katibu Mkuu wa CUF, amewataka wanachama na viongozi wa chama hicho kwa dhati kuwa imara ili kukabiliana na watu hao.
Akitaja sababu kwa CCM na washirika wake kuanza kuweweseka, amesema uamuzi huo umetokana na kufanyika utafiti maalum kuhusu hali ya kisiasa na nguvu za vyama zilivyo kuelekea Uchaguzi Mkuu ujao Zanzibar.
“Utafiti huo ulionesha, kwamba CCM inaungwa mkono kwa asilimia 36 tu ya wananchi wa Zanzibar, huku ACT – Wazalendo ikiungwa mkono na asilimia 64 ya wananchi wa Zanzibar. Hali hii imewatia hofu,” amesema.
Leave a comment