MAALIM Seif Sharif Hamad, mshauri mkuu wa Chama cha ACT-Wazalendo, amechukua fomu ya kugombea nafasi ya uenyekiti wa chama hicho. Anaripoti Jabir Idrisa, Zanzibar…(endelea).
Kiongozi huyo nguli wa siasa za upinzani Zanzibar, amechukua fomu hiyo leo tarehe 30 Januari 2020, katika ofisi ndogo za chama hicho zilizopo Vuga, Unguja.
Doroth Semu, Kaimu Katibu Mkuu wa chama hicho ndiye aliyemkaribisha na kumkabidhi fomu Maalim Seif, huku akisema ‘nafasi zipo wazi kwa kila mwanachama aliyetimiza vigezo.’
Chama hicho, tarehe 27 Januari 2020, kilifungua mlango kwa wanachama wake walio na sifa, kujitokeza na kuchukua fomu za kugombea nafasi mbalimbali za uongozi ndani ya chama hicho.
Mbele ya vyombo vya habari, Maalim Seif amesema, amejitokeza kuchukua fomu hiyo kwa kuwa, ana haki ya kufanya hivyo kama ilivyo kwa wanachama wengine wa chama hicho.
Na kwamba, anao uwezo na uzoefu wa muda mrefu katika masuala ya siasa na uongozi, hivyo anaamini nafasi hiyo ni muafaka kwake hasa katika kipindi hiki.
Amesema, kujitokeza kwake kuchukua fomu hiyo kunatokana na malengo yake ya kufanyia mabadiliko makubwa ya chama hicho, “kama wanachama wataniridhia kuwa mwenyekiti, nitasimamia uwajibikaji na nidhamu ndani ya chama.”
Leave a comment