WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola amewaelekeza wakuu wote wa vyombo vya Ulinzi na Usalama nchini kuainisha maeneo yote ya ardhi wanayomiliki ili kuepusha uvamizi wa maeneo hayo kwa baadhi ya wananchi na makampuni mbalimbali. Anaripoti Khalifa Abdallah … (endelea).
Lugola amesema kuwa ameagiza wakuu wa vyombo hivyo vya ulinzi kuainisha maeneo yaliyopimwa na yenye hati miliki na kuainisha maeneo ambayo yana migogoro na wananchi ama taasisi pamoja na hatua ambazo zimefikiwa katika kushughulikia migogoro hiyo.
“Kumekuwa na tabia ya baadhi ya wananchi na makampuni mbalimbali kuvamia maeneo yanayomilikiwa na majeshi yaliyoko ndani ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi na kufanya shuguli mbalimbali za uzalishaji ikiwemo kilimo, ufugaji na hata kuanzisha viwanda, kuanzia leo ni marufuku kwa mwananchi, kampuni au shirika kuvamia maeneo yanayomilikiwa na vyombo vya Ulinzi na Usalama likiwemo Jeshi la Polisi, Magereza, Zimamoto na Uokoaji, Uhamiaji na mtu yoyote atakayebainika kufanya hvyo atachukuliwa hatua za kisheria,” amesema.
Katika hatua nyingine, Lugola ameagiza Jeshi la Polisi kitengo cha usalama barabarani kuweka utaratibu maalum wa kukamata magari hasa yakiwa na abiria kunakopelekea kuwachelewesha abiria hao katika shughuli zaidi huku wakiwa hawana hatia yoyote.
Lugola ameagiza kuwepo na utartibu wa kutokamatwa kwa magari yanapofanya makosa yakiwa na abiria badala yake yaachwe hadi yafike mwisho wa safari na yashushe abiria na ndio dereva akamatwe.
“Nimemuelekeza Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchini kuhakikisha jambo hili halitokei tena, kwa mfano leo nimepigiwa simu baadhi ya abiria wakilalamika kufanyiwa jambo hilo na askari aliyewakamata akawaacha kituoni na akaenda zake,” amesema.
Leave a comment