EDWARD Lowassa, Waziri Mkuu Mstaafu, amekwepa kuzungumzia hatua ya Frederick Sumaye, kujitenga na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema). Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Sumaye, aliyekuwa Mwenyekiti wa Chadema, Kanda ya Pwani na Waziri Mkuu Mstaafu (1995-2005), alitangaza kuachana na chama hicho jana tarehe 4 Desemba 2019, kwa madai ya kushindwa kile alichoita vitimbi ndani ya chama hicho.
Akizungumza na kituo cha EATV leo tarehe 5 Desemba 2019, Lowassa aliulizwa ushauri au maoni yake kuhusu hatua ya Sumaye kuachana na Chadema.
Lowassa amesema, “kuhusiana na suala hilo, kwa sasa mimi siwezi kuzungumza chochote, nadhani ungeniacha tu,” amesema Lowassa.
Lowassa ni miongozi na wanasiasa walioikimbia Chadema, tarehe 1 Machi 2019, mwanasiasa huyo na mbunge wa zamani wa Monduli, alitangaza kurejea CCM ambapo alipokewa na Dk. John Magufuli, Mwenyekiti wa CCM, kwenye ofisi ndogo za chama hicho – Lumumba.
“Nimetafakari na nimeamua kurudi nyumbani,” alisema Lowassa mbele ya Dk. Magufuli na viongozi wengine wa CCM.
Lowassa aliondoka CCM na kujiunga Chadema wakati wa mchakato wa kuelekea Uchaguzi Mkuu mwaka 2015. Ilikuwa baada ya jina lake kukatwa katika kugombea urais kupitia CCM.
Hata hivyo, alipata ridhaa ya kugombea urais kupitia Chadema na kuungwa mkono na vyama vinne vya siasa vilivyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA).
Imeelezwa, kujing’atua kwa Sumaye ndani ya Chadema, kumechagizwa na uamuzi wake wa kuchokonoa nafasi ya uenyekiti Taifa, nafasi hiyo inashikwa na Freeman Mbowe kwa miaka 15 sasa.
Iwapo Mbowe atachaguliwa tena kuwa mwenyekiti, atafikisha miaka 20 madarakani.
Leave a comment