TUNDU Lissu, Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maaendeleo (Chadema)-Bara amesema, atazungumza na Watanzania Jumatatu tarehe 8 Juni 2020 kuelezea adhima yake ya kuwania urais ndani ya chama hicho. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Amesema, atazungumza na wananchi kupitia mtandao wa facebook. “Nitazungumza na Taifa Jumatatu, 8 Juni, 2020 kupitia Facebook Live Streaming.”
Lissu ni miongoni mwa makada wa Chadema, ambao wameweka wazi nia ya kuomba ridhaa ya chama hicho kimpitishe ili kuwania urais wa Tanzania katika uchaguzi mkuu Oktoba 2020.
Juzi Jumatano tarehe 3 Juni 2020, Katibu Mkuu wa Chadema, John Mnyika alitangaza kufunguliwa kwa milango ya makada wa chama hicho wanaotaka kuwania urais kuandika barua kwenda ofisini kwake.
Mnyika alisema, milango hiyo itakuwa wazi hadi tarehe 15 Juni 2020 huku Lissu siku hiyo hiyo akiieleza MwanaHALISI ONLINE kwamba atatia nia na muda mwafaka ukifika ndani ya kipindi hiko, atazungumza na Watanzania na wadau wengine.
Leo Ijumaa tarehe 5 Juni 2020 kupitia ukurawake wake wa Twitter, Lissu amesema atazungumza na Jumatatu moja kwa moja kupitia Facebook.
Nitazungumza na Taifa Jumatatu, 8 June, 2020 kupitia Facebook Live Streaming.
14:00 EAT 13:00 CET 7:00AM EST (USA) pic.twitter.com/BQ64poXbvF
— Tundu Antiphas Lissu (@TunduALissu) June 5, 2020
Lissu amekuwa nje ya Tanzania tangu tarehe 7 Septemba 2017, aliposafirishwa kwenda Hospitali ya Nairobi, Kenya kwa matibabu baada ya kushambuliwa kwa risasi zaidi ya 30 nje ya makazi yake Area D jijini Dodoma.
Mwanasiasa huyo alifikwa na mkasa huo, akitoka kuhudhuria vikao vya Bunge lililokuwa likiendelea jijini humo.
Alipata matibabu Nairobi hadi tarehe 6 Januari 2018 alipohamishiwa Ubelgiji aliko mpaka sasa kwa matibabu zaidi.
Hata hivyo, Lissu amekwisha kusema, amepona na anachosubiri ni kuhakikishiwa mazingira salama ya maisha yake ili yasije kujitokeza kama yaliyomkuta awali.
Chini ya ujumbe huo wa Lissu, watu mbalimbali wamechangia kwa waliopongeza na kumpinga juu ya hatua hiyo.
Leave a comment