TUNDU Lissu, aliyekuwa mgombea urais kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), ametoa masharti matatu ili arejee nchini. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Akijibu swali lililomtaka kueleza ni lini atarejea nchini Tanzania, Lissu amesema ni mapema kwa sasa kusema lini atarejea Tanzania na kwamba, kilichomfanya aondoke ni baada ya kutishiwa usalama wa maisha yake.
Ametoa masharti hayo ikiwa ni siku nne kupita baada ya Mkuu wa Jeshi laPolisi nchini, IGP Simon Sirro kumtaka Lissu na Godbless Lemba, aliyekuwa mbunge wa Arusha Mjini kurejea nchini na kwamba, atawalinda.
“Nchi yetu ya amani na utulivu na kama wako nje warudi nchini kuna amani. Ni vizuri Watanzania wakaelewa kwamba, hili ni suala la mtu binafsi anaamua kusema tu. Kimsingi tukipata taarifa hiyo niko tayari kumpa ulinzi na familia yake, ataishi kwa amani,” alisema IGP Sirro.
Na hata Lissu alipoulizwa, anataka uhakika gani kwa jeshi la polisi ili arejee Tanzania, ametaja mambo matatu kwamba, yakitekelezwa anaweza kurejea nchini.
“…kwanza kesi zote za jinai ziondolewa bila masharti yoyote, pili lazima waseme nani alinipiga risasi na pia waeleze zile kamera za CCTV zilipelekwa wapi?” amesema Lissu leo tarehe 23 Novemba 2020 katika mkutano wake na wanahabari uliofanyika mtandaoni.
Amesema, Desemba mwaka jana chama chake – Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) – kilimwandikia barua nia yake ya kurejea nchini na kutaka uhakika wa uslama wake, hata hivyo barua hiyo haikujibiwa.
“Desemba mwaka jana tuliandika barua kwa IGP, kumueleza niko tayari kurejea nyumbani, nahitaji usalama kutokana na tishio lakini haijajibiwa, Januari tulikumbusha lakini hatukujibiwa,” amesema Lissu ambaye ni Makamu Mwenyekiti wa Chadema.
Akisisitiza sababu za yeye kurejea, amesema atafanya hivyo iwapo tu jambo la msingi kwake – usalama wake – vitazingatiwa Tanzania hasa baada ya kutishiwa maisha yake baada ya uchaguzi mkuu.
“Lini nitarudi…? Nimekuwepo hapa (Ubelgiji) kwa siku hapa 12 tu, sijamaliza hata karantini ya siku 14, ni mapema kusema lini nitarudi. Inategemea na jambo moja muhimu, uhakika wa usalama wangu na maisha yangu.
“…sijakimbia, nimejiokoa maisha yangu, nimejaribiwa kuuawa miaka mitatu iliyopita lakini sasa nitarejea pale tu mazingira yatakuwa salama,” amesema.
Akijibu swali kuhusu kesi zake mahakamani, Lissu amesema kama mahakama iliweza kumsubiri kwa miaka mitatu mpaka akarejea, pia inaweza kumsibiri kwa kipindi kingine kijacho.
“Kesi zitanisubiri, kama walinisubiri kwa miaka mitatu, wanaweza kunisubiri zaidi, kitu muhimu kwangu ni usalama wangu,” amesema.
Aendelee kubaki hukohuko hao was belgiji wanapenda ushoga …………
Upo sahihi kabisa Lissu . Wanawezaje kukuhakikishia usalama ukirudi wakati hawajui nani aliyekushambilia mwaka 2017 mchana kweupe!!