TUNDU Antipus Lissu, amependekezwa na wajumbe wa Baraza Kuu la Chama cha Demokarsia na Maendeleo (Chadema) kuwa mgombea urais wa chama hicho katika Uchaguzi Mkuu wa Tanzania utakaofanyika Jumatano tarehe 28 Oktoba 2020. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.
Msimamizi wa uchaguzi huo ambaye ni John Mnyika, Katibu Mkuu wa Chadema amesema, Lissu amepata kura 405 ya kura zote 442 za wajumbe waliopiga kura leo Jumatatu katika ukumbi wa Mlimani City jijini Dar es Salaam.
Lazaro Nyalandu ambaye ni mwenyekiti wa Chadema Kanda ya Kati ambaye amewahi kuwa waziri wa maliasili na utalii, ameshika nafasi ya pili kwa kura 36 na Dk. Mayrose Majinge kura moja.
Amesema jina la Lissu ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa Chadema Bara litapelekwa kesho Jumanne tarehe 4 Julai 2020 katika mkutano mkuu wa chama hicho kwa ajili ya kuthibitishwa.
Wakati, Mnyika akitangaza matokeo hayo, shangwe zililipuka ukumbini mzima kwa nyimbo na shangwe mbalimbali.
Ikiwa, mkutano mkuu huo utampitisha, Lissu anakwenda kuchuana na mgombea wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais John Pombe Magufuli ambaye naye amekwisha kupitishwa na chama chake.
Wagombea wengine wa urais na vyama vyao kwenye mabano ni, Profesa Ibrahim Lipumba (CUF), Hashimu Rungwe (Chaumma) na John Shibuda wa Ade- Tadea.
Leave a comment