MBUNGE wa Chadema katika jimbo la Moshi Vijijini, Anthony Bahati Komu, ametinga nchini Ubelgiji ili kumjulia hali mbunge mwenzake wa Singida Mashariki, Tundu Lissu. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Lissu yuko nchini Ubelgiji anakopatiwa matibabu na madaktari bingwa wa mifupa katika hospitali ya chuo kikuu cha Luvein, kilichopo nchini humo.
Taarifa kutoka Luvein zinasema, mbali na kumjulia hali Lissu, viongozi hao walipata nafasi ya kujadiliana mambo mbalimbali, ikiwamo gharama za matibabu yake na mwenendo wa demokrasia nchini.
Katika mazungumzo hayo, Lissu alimshukuru Komu na wenzake wengine sita kwa kile alichoita, “kufanya maamuzi ya busara” ya kumuondoa Nairobi kumpeleka nchini Ubelgiji.
Alisema, “nakushukuru sana kaka wewe na wenzako kwa uamuzi wenu wenye busara wa kuniondoa Nairobi na kunileta hapa kupata matibabu bora zaidi, kulinganisha na yale ambayo nilikuwa nayapata pale Nairobi.
Lissu anatarajiwa kufanyika upasuaji mwingine mkubwa wa 24 wiki mbili zijazo. Upasuaji huo unafanyika kufuatia madaktari wanaomtibu, kufanikiwa kutokomeza bakteria waliokuwa wameshambulia sehemu za mwili wake.
“Natarajiwa kufanyiwa upasuaji mwingine mkubwa wiki mbili zijazo. Upasuaji huu unafanyika kwenye goti hadi kwenye nyonga. Madaktari wameniambia kuwa upasuaji wa safari hii, utachukua muda wa saa sita,” amenukuliwa Lissu akimueleza Komu.
Anasema, upasuaji huo unafanyika katika maeneo ambayo nilifanyiwa operesheni Nairobi. Nilipofika hapa madaktari waliona kuna shida kidogo na hivyo, wameamua kufanya operesheni upya.”
Kwa mujibu wa Lissu, alipofika nchini Ubelgiji, madaktari wake wanaomtibu waligundua kuwapo hitilafu kwenye mguu wangu wa kulia; baada ya uchunguzi wameamua kufanyika kwa operesheni upya.
Lissu yuko Ubelgiji kwa takribani miezi mitano sasa, kufuatia kushambuliwa kwa risasi, nje ya nyumba yake, Area D, mjini Dodoma. Alikuwa akirejea nyumbani kutokea bungeni.
Mwanasiasa huyo ambaye ni Mnadhimu wa Kambi rasmi ya upinzani bungeni na mwanasheria mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo, alinusurika kifo, wiki mbili baada ya kunukuliwa akisema, “maisha yangu yako hatarini.”
Lissu alikwenda kwenye matibabu nchini Ubelgiji, tarehe 6 Januari mwaka huu.
Akizungumzaa kwa njia ya simu na mwandishi wa gazeti hili kutoka *** Komu amesema, “amebakiza operesheni moja. Baada ya hapo ataendelea kuwapo hospitali kwa ajili ya mazoezi kabla ya kurejea nchini.”
Hata hivyo, Komu hakueleza lini Lissu anatarajiwa kurejea nyumbani.
“Haijajulikana atarejea lini. Tunachohang’aika nacho kwa sasa ni matibabu yake. Lakini fahamu kuwa Lissu hawezi kuishi uhamishoni. Atarejea Tanzania kuja kujenga nchi yake na kuwatumikia wapiga kura wake,” amesisiza Komu.
Kauli ya Komu kuwa ni lazima Lissu atarejea nchini baada ya matibabu yake, inaweza kuwa imemaliza minong’ono ya chini kwa chini inayodai kuwa kuna shinikizo kutoka kwa baadhi ya ndugu zake kumtaka asirudi Tanzania.
Leave a comment