Thursday , 28 March 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Lissu akamatwa tena, polisi watoa ufafanuzi
Habari za SiasaTangulizi

Lissu akamatwa tena, polisi watoa ufafanuzi

Tundu Lissu, Mwanasheria Mkuu wa Chadema akizungumza na waandishi wa Habari (hawapo pichani)
Spread the love

SIKU moja baada ya polisi kumhakikishia Tundu Lissu, Mwanasheria Mkuu wa Chadema kuwa yupo huru na hakuna mpango wa kumkamata, hatimaye leo Jeshi la Polisi jijini Dar es Salaam limemkamata akiwa uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Nyerere (JKNIA), anaandika Charles William.

Lissu amekamatwa akiwa uwanjani hapo tayari kwa safari ya kuelekea jijini Kigali, Rwanda kuhudhuria kikao cha halmashauri ya vyama vya mawakili wa Afrika Mashariki (EALS).

“Nipo uwanja wa ndege, najiandaa kuelekea Kigali kwenye kikao cha halmashauri ya EALS kinachoanza kesho. Watu waliojitambulisha kama maafisa kutoka ofisi ya Mkuu wa upelelezi Dar wamekuja kunikamata ili kunipeleka Kituo Kikuu cha Polisi,” amesema Lissu kupitia ujumbe alioutoa kupitia mitandao ya kijamii.

Taarifa ya polisi kumsaka Lissu kwa lengo la kumkamata zilizanza kusikika tangu Jumatano, ambapo Lissu akiwa katika kazi zake za uwakili mkoani Dodoma alielezwa kuwa maofisa wa Polisi walikuwa wakimsubiri nje ya chumba cha mahakama ili wamkamate.

Hata hivyo, Lazaro Mambosasa Mkuu wa Polisi Mkoa wa Dodoma alimfuata katika chumba hicho cha mahakama ambacho Lissu alieleza kuwa asingetoka nje na kumtaarifu kuwa jeshi la polisi mkoani Dodoma na hata makao makuu halina mpango wa kumkamata.

“Mimi sina maagizo ya kukukamata na wala IGP (Inspekta Jenerali wa Polisi), hajatoa maagizo ya kukukamata…. upo huru,” alieleza Kamanda Mambosasa.

Masaa 24 baada ya kauli hiyo ya polisi, Lissu amejikuta yupo nguvuni huku Lucas Mkondya, Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam akiueleza mtandao wa MwanaHALISI online kuwa Lissu amekuwa akitafutwa ili kuhojiwa.

“Sasa hivi sipo ofisini, sijajua kama tumempata lakini tulikuwa tunamtafuta kwa ajili ya mahojiano, kuna vitu tunataka atuambie. Hatuwezi kukwambia kwa sasa ni vitu gani tunataka tumhoji, lakini tukimpata na kumhoji tutakwambia,” ameeleza kwa njia simu.

Kukamatwa kwa Lissu, kunaweza kuhusishwa na kauli alizozitoa Jumatatu ya wiki hii tarehe 17 Julai, 2017 katika mkutano wake na wanahabari Kinondoni, jijini Dar es Salaam ambapo pamoja na mambo mengine alimtuhumu Rais John Magufuli kuwa anaendesha nchi kidikteta.

“Nani anayeweza kutuambia, uwanja wa ndege wa Chato unajengwa kwa gharama gani na ilipitishwa na nani. Nani anayejua ndege za Bombadia zimenunuliwa kiasi gani na ziliidhinishwa na nani na kwa utaratibu gani?

“Leo hii, nani anayeweza kubisha kuwa Rais Magufuli anaendesha nchi kwa misingi ya upendeleo wa kifamilia, kikabila na kikanda? Amemteua Katibu Mkuu Wizara ya Fedha ambaye ni mtoto wa dada yake ili anapotaka fedha, mpwa wake ambaye ni mlipaji mkuu wa serikali awe anatoa kiurahisi,” alisema Lissu.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za SiasaMakala & Uchambuzi

Nani anasema kuna hasara ATCL?

Spread the loveRIPOTI za makusanyo na matumizi ya fedha katika Kampuni ya...

Habari za SiasaTangulizi

CAG: Wastaafu, wenza wao chanzo NHIF kufilisika

Spread the loveRIPOTI ya ukaguzi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu...

Habari za SiasaTangulizi

Vikundi hewa 851 vyalamba bilioni 2.6 mikopo ya halmashauri

Spread the loveVIKUNDI hewa vya wajasirimali wadogo 851 kutoka katika halmashauri 19...

Habari za SiasaTangulizi

Mashirika matano yapata hasara mabilioni ya fedha

Spread the loveMASHIRIKA matano ya Serikali yanayojiendesha kibiashara, yamepata hasara ya mabilioni...

error: Content is protected !!