Friday , 19 April 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Lissu aeleza atakayofanya 2020-2025
Habari za SiasaTangulizi

Lissu aeleza atakayofanya 2020-2025

Spread the love

TUNDU Lissu, mgombea urais wa Tanzania kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) amesema, misingi ya Ilani ya Uchaguzi ya chama hicho 2020/25 imejengwa na uhuru, haki na maendeleo ya watu. Anaripoti Faki Sosi, Dar es Salaam…(endelea)

Lissu alisema hayo jana Jumamosi tarehe 29 Oktoba 2020 kwenye viwanja vya Tanganyika Pakers jijini Dar es Salaam katika siku ya pili kati ya tatu ya kampeni jijini humo.

Kabla ya kuanza kuzungumza, Freeman Mbowe, Mwenyekiti wa Chadema, aliwakabidhi Lissu na mgombea wake mwenza, Salum Mwalimu Ilani ya Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Jumatano tarehe 28 Oktoba 2020 ya chama hicho ambayo watainadi kwa Watanzania.

Katika hotuba yake, Lissu alisema, mbali na kuweka misingi hiyo kwenye ilani hiyo, alisema ili afanikishe hayo yote ni lazima wananchi wafanye mabadiliko ya kisiasa ya kikataba.

Akizungumzia mabadiliko ya kikatiba, Lissu alisema, nchi ili irejee kwenye misingi yake ni lazima kupatikane kwa Katiba Mpya na akianzia “pale ulipoishia mchakato wa katiba ya Jaji Warioba.”

Wakati huo huo, Lissu aliweka wazi sera zake ambapo ameainisha Serikali yake itapunguza kiwango cha kodi kwa wafanyabiashara, itawapa nafuu ya mikopo ya elimu ya juu wanafunzi, itahakikisha kila mwananchi anakuwa na bima ya afya.

Kuhusu uhuru, haki na maendeleo ya watu akirejea alichowahi kusema Hayati Mwalimu Julius Kambarahe Nyerere, Rais wa kwanza wa Tanzania kuwa alihimiza maendeleo yanayogusa maisha ya watu.

“Maendeleo yanayoumiza watu, maendeleo yanayoumiza watu ni maendeleo ambayo sisi tunayokaa sasa, maendeleo tunayoyataka yanayozingatia uhuru wa watu, haki zao, maendeleo aliyoyaita Baba wa Taifa maendeleo ya watu badala ya maendeleo ya vitu,” alisema Lissu huku akishangiliwa uwanjani hapo

Lissu ambaye kitaalamu ni mwanasheria alisema, Serikali ya Chadema itakuwa ya maridhiano ya kitaifa, itawalipa fidia itakayowatosheleza wale wahanga wa bomobomoa.

Alisema, Jiji la Dar es Salaam ni Jiji muhimu kiuchumi na kibiashara na viwanda kuliko pahala popote nchini.

Alisema, wanafanyabiashara wa Tanzania na Dar es Salaam wanakabiliwa na wingi wa kodi zinazorejesha nyuma maendeleo yao.

Alisema, Serikali ya Chadema itatoa nafuu wananchi kwenye kulipa kodi.

“Mpango wetu ni kupunguza kodi, kuondoa huu utitiri wa kodi, tuwe na kodi moja ambayo ukilipa hakuna atakayekubugudhi tena,” alisema Lissu.

“Mfumo wa kodi utakuwa wa haki ya mlipa kodi, badala ya kufilisi watu biashara zao sisi tutastawisha walipa kodi.”

Kuhusu wafanyakazi, Lissu alisema, Serikali yake itaongeza maslahi kwa wafanyakazi nchini.

“Nchi hii kwa miaka mitano haijaongeza mshahara kwa wafanyakazi kwa miaka mitano wakati sheria yetu inasema, kila mwaka wafanyakazi waongozewe mishahara.”

“Sisi Chadema mkitupa ridhaa, tutalipa fidia ya mishahara ya wafanyakazi kwa miaka mitano,” alisema Lissu.

Akizungumzia suala la mafao, alisema Serikali yake itarejesha kwa wafanyakazi fao la kujitoa.

Lissu alisema, Serikali yake itarejesha ulipaji wa mikopo kwa wanafunzi wa elemu ya juu ile ya asilimia tatu badala ya asilimia 15 ya sasa jambo linalowafanya wanufaika kusota kuilipa.

“Msingi wa uchumi utakuwa uchumi huru, uchumi wa sekta binafsi, tutahakikisha kwamba wale wanaofaa kufungua viwanda hawana hofu ya kunyang’anywa viwanda vyao.”

“Zama za serikali kuhodhi kila kitu zishapita na hairudi tena miaka mitano hii tumeshuhudia serikali hii ikirejesha ujamaa,” alisema

Lissu alisema “Serikali nitakayokuwa ninayoiongoza mimi, masuala ya ujenzi yatakuwa yanasimamiwa na sekta binafsi.”

Kuhusu afya, Lissu alisema akiingia madarakani atahakikisha kila mwananchi anamiliki bima ya afya.

“Mimi nimekaa hospitalini muda mrefu, nimetibiwa kwenye hospitali bora kabisa, nitatengeneza mfumo bora kwa kuhakikisha kila mtu anakuwa na bima ya afya,” alisema

Kuhusu elimu, alisema mfumo wa elimu umejengwa kwenye mfumo wa ‘pasi mtihani’ tumejenga taifa la vijana ambao kazi yao ni kufaulu mitihani tu kwa sababu mfumi wetu wa elimu hautoi maarifa.

“Tutabadilisha falsafa ya elimu ya Tanzania ili iwafanye waweze kuajirika, tunashindwa kushindana kwenye soko la ajira na vijana wa nchi nyengine,” alisema

Lissu leo Jumapili atakuwa Uwanja Shule ya Msingi Liwiti Tabata jijini Dar es Salaam.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

KimataifaTangulizi

Mkuu wa majeshi Kenya afariki, Ruto atangaza maombolezo

Spread the loveRais wa Kenya, William Ruto ametangaza maombezo ya siku tatu...

Habari za SiasaTangulizi

Tanzania, Uturuki zanuia kukuza biashara, uwekezaji

Spread the loveSERIKALI za Tanzania na Uturuki zimekubaliana kuendeleza dhamira ya kuimarisha...

Habari za Siasa

Tume huru ya uchaguzi yatangaza ajira watendaji daftari wapiga kura

Spread the love  TUME Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), imetangaza nafasi...

Habari za SiasaTangulizi

Chadema yatangaza ruti awamu ya pili maandamano

Spread the love  CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimesema awamu ya...

error: Content is protected !!