TUNDU Antipas Lissu, Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), amechukua fomu ya kugombea urais wa Tanzania, kupitia chama hicho, katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2020. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Fomu hiyo imechukuliwa leo Jumamosi tarehe 4 Julai 2020 katika Ofisi za Makao Makuu ya Chadema jijini Dar es Salaam, na David Jumbe, wakala wa Lissu.
“Nimekuja kwa ajili ya kuchukua fomu kama wakala wa Tundu Lissu, mnafahamu Lissu yuko nje ya nchi.”
“Tukitoka hapa, tutaanza kazi ya kujaza na kutafuta wadhamini na kwa mujibu wa maelekezo, tupate wadhamini 100 kwa kila kanda. Tukitoka hapa tutaanza Kanda ya Pwani,” amesema Jumbe.
Soma zaidi:-
-
Lissu: Narejea Tanzania kabla ya Julai 28
-
Wakili Alute: Hakuna kikwazo Lissu kugombea Urais akiwa ughaibuni
-
Lissu amwomba Rais Magufuli ajiandae kumpokea
Jumbe amesema, Lissu anafaa kuwa mgombea urais wa Chadema kwa kuwa, anaushawishi kwa wananchi pamoja na kutokuwa na kashfa.
“Tunamhitaji Lissu kwa nchi yetu sababu miaka mitano katiba na sheria za nchi zimekiuka, watumishi wamekuwa wakifanya kazi kwa maagizo na si kwa taaluma na maadili zao.”
“Sisi tunaamini Lissu anakwenda kunyoosha nchi, watu wafanye kazi kwa kufuata kanuni na miongozo na si kufanya kitu kwa kutegemea kichwa cha mtu mmoja,” amesema Jumbe.
“Hana kashfa na Watanzania wanaamini ni mtu sahihi anayeweza kumuondoa Rais John Magufuli katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2020,” amesema.
Jumbe amemchukulia fomu Lissu ambaye yuko nje ya Tanzania tangu tarehe 7 Septemba 2017 aliposhambuliwa na watu wasiojulikana kwa risasi zaidi ya 30 akiwa katika makazi yake Area D jijini Dodoma.
Siku hiyohiyo usiku, alihamishiwa Hospitali ya Nairobi nchini Kenya kwa matibabu hadi tarehe 6 Januari 2018 alipopelekwa nchini Ubelgiji kwa matibabu zaidi.
Chadema kimefungua zoezi hilo leo kwa watia nia wa kugombea urais wa Tanzania na Zanzibar, ubunge, uwakilishi na udiwani.
Zoezi la uchukuaji fomu ya kugombea urais litafika tamati tarehe 19 Julai 2020, wakati kwa wagombea ubunge, udiwani na uwakilishi lotafungwa tarehe 10 Julai 2020.
Tarehe 28 na 29 Julai 2020, mkutano wa Baraza Kuu na Mkutano Mkuu utafanyika ili kumpata mgombea Urais.
Endelea kufuatilia MwanaHALISI Online & MwanaHALISI TV kwa habari zaidi
Leave a comment