CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimesema, kitambadilishia majukumu Tundu Lissu, Mgombea wake wa Urais wa Tanzania wakati akiitumikia adhabu ya kutofanya kampeni kwa muda wa siku saba kuanzia jana tarehe 3 hadi 9 Oktoba 2020. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam….(endelea).
Kamati ya Maadili ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi nchini Tanzania (NEC) tarehe 2 Oktoba 2020 ilimpa adhabu hiyo Lissu baada ya vyama vya NRA na CCM kuwasilisha malalamiko kuwa ametoa maneno ya uchochezi yaaiyothibitika.
Akizungumza na wanahabari leo jumapili tarehe 4 Oktoba 2020 jijini Dar es Salaam, Freeman Mbowe, Mwenyekiti wa Chadema amesema, mbadala wa Lissu kutofanya kampeni za Uchaguzi Mkuu wa tarehe 28 Oktoba 2020 katika kipindi hicho, mwanasiasa huyo atapangiwa kazi maalum kama Makamu Mwenyekiti wa Chadema-Bada
“Tumemshauri mgombea wetu, Tundu Lissu hatoendelea na kampeni zake. Lissu ni makamu mwenyekiti, kuna majukumu mengi ya kufanya na sisi tutampangia kazi ya kufanya katika kipindi cha siku saba.”
“Hatoendelea na kampeni ila atafanya majukumu mahususi kama makamu mwenyekiti, sasa tuone watasemaje tena,” amesema Mbowe.
Aidha, Mbowe amesema, Kamati Kuu ya Chadema imeelekeza Kitengo cha Sheria cha chama hicho kuandaa hati ya dharura kwa ajili ya kufungua kesi mahakamani kuipinga adhabu hiyo.
Hata hivyo, Mbowe amesema, uamuzi wa kesi hiyo hata kama utacheleweshwa, lakini utaweka historia sawa.
“Sisi kama Chadema, tunapinga adhabu aliyopewa Tundu Lissu na tumeelekeza kitengo chetu cha sheria kwa hati ya dharura kufungua kesi Mahakama Kuu kupinga uamuzi huu wa kumsimamishwa. Najua uamuzi unaweza kuchelewa kutolewa lakini tunaweka rekodi sawa,” amesema Mbowe.
Leave a comment