SAED Kubenea, Mbunge wa Ubungo (Chadema) amemtuhumu Dk. Phillip Mpango, Waziri wa Fedha na Mipango kwamba, ameshindwa kumsaidia Rais John Magufuli kuimarisha uchumi wa nchi. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Amesema, pamoja na Dk. Mpango kuwa na uzoefu wa masuala ya kuchumi, alipokuwa Katibu wa Tume ya Mipango katika Serikali ya Awamu ya Nne, ameshindwa kutumia ujuzi huo kuitoa nchi hapa ilipo kiuchumi.
Akihojiwa na Kituo cha Televisheni cha ITV leo tarehe 13 Juni 2019 katika kipindi cha Kumekucha, Kubenea amesema, kutokana na uzoefu wa Dk. Mpango katika masuala ya uchumi na mipango, kama angemshauri vyema Rais Magufuli, mazingira ya bishara yasingesinyaa kama ilivyo sasa.
“Nashangaa sababu za Waziri Mpango kushindwa kuokoa uchumi wan chi hii, nashangaa sababu yeye alikuwa Katibu wa Tume ya Mipango wakati wa Kikwete, ningetarajia angemshauri vizuri rais. Angeweza kumuongoza vizuri rais ambaye si mzuri katika masuala ya uchumi,” amesema Kubenea na kuongeza;
“Lakini badala yake mwaka wa nne katika utekelezaji wa bajeti, serikali inakuja kutengeneza mazingira mazuri ya biashara, mi nilitarajia mazingira mazuri ya biashara yangekuwepo tangu mwanzo, na kama tungeyaendeleza, tungekuwa mbali sana.”
Kuhusu bajeti inayotarajiwa kusomwa leo jioni bungeni jijini Dodoma, Kubenea amesema, bado kuna changamoto ya serikali kufikia malengo yanayokusidiwa ukilinganisha na hali ya uchumi wa nchi ilivyo.
Kubenea amesema matarajio yake ni kuona kwamba serikali itakuja na kodi za miaka nyuma, kwa kuwa haijaweka nguvu katika kuhakikisha bajeti ya mwaka huu inafuta kasoro za bajeti iliyopita.
“Matarajio yangu ni kwamba, serikali itakuja na kodi zile zile ya miaka ya nyuma, sababu mfumo mzima wa ulipaji kodi umevurugika kwenye nchi hasa kwenye sekta binafsi, katika kipindi hiki cha miaka mitatu imevurugika sana.
“…tulikuwa tunategemea kupata fedha kutoka sekta ya madini, sasa hivi migodi inafungwa, walipa kodi kama bureau de change nazo zimetikisika, sioni mahala ambapo serikali itakusanya trilioni 33 na ikatekeleza bajeti yake kikamlifu, na hata ukiangalia bajeti inayoisha utekelezaji wake chini ya silimia 70,” amesema.
Aidha, amesema serikali haiwezi kujiendesha kwa kutegemea kodi za wafanyabiashara pekee, nashauri iwekeze katika miradi ya mikakati.
“Tungeweza kuwekeza fedha za kutosha kwenye viwanda, kilimo mazao ya biashara bidhaa zingezalishwa, tungepata kodi, waajiriwa wangepata kodi, wafanyakazi wangekunywa chai kwa mama lishe, naye atanunua ngano na atalipa kodi,” amesema Kubenea.
Leave a comment