SAED Kubenea, Mbunge wa Ubungo (Chadema) ameihoji serikali kwamba, ni lini itafufua nakuwa imara zaidi Kiwanda cha Urafiki ili kifanye kazi kwa maslahi ya wananchi na taifa kwa ujumla kama ilivyokusudiwa? Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma…(endelea).
Akizungumza bungeni leo tarehe 8 Februari 2019 Kubenea amesema, kiwanda hicho cha nguo kilichopo katika Jimbo la Ubungo jijini Dar es Salaam ni miongoni mwa viwanda vilivyobinafsishwa na serikali.
“Katika kiwanda cha nguo cha Urafiki mwekezaji hakuja na mtaji badala yake serikali ilienda kukopa katika Benki ya Exim ya China na ikampa mwekezaji mtaji wa kuendesha Kiwanda cha Urafiki mikononi mwa wananchi wa Dar es Salaam,” amesema.
Akijibu swali hilo Injinia Stella Manyanya, Waziri wa Viwanda na Biashara amesema, kiwanda hicho msingi wake ni uhusiano kati ta China na Tanzania.
“Kama ambavyo amezungumza Kiwanda cha Urafiki ni uhusiano kati ya Nchi ya China na Tanzania. Ni kiwanda ambacho kilijengwa msingi wake ni mahusiano ya nchi hizo mbili kidiplomasia.
“Hivyo basi, tunatamani kuona kiwanda hicho kikifanya kazi vizuri zaidi na wote tumefuatilia na kujua maeneo yanayohitajika kufanyiwa marekebisho,” amesema Injinia Manyanya.
Amesema, kuwa serikali zote mbili zinashughulika kwa pamoja kuona namna gani kiwanda hicho kinaweza kuendeshwa kisasa zaidi.
Waziri huyo amesema, katika kujenga uchumi wa viwanda, Serikali ya Awamu ya Tano tangu iingie madarakani hadi kufikia Desemba Mwaka 2018, jumla ya viwanda 3,504 vimeanzishwa nchini.
Amefafanua kuwa, viwanda hivyo vinajumuisha viwanda vidogo sana 2500, viwanda vidogo 943, viwanda vya kati 51 na viwanda vikubwa 10.
“Wizara yangu kwa kushirikiana na Ofisi ya Msjili wa Hazina imekuwa ikifanya tathmini ya viwanda 156 vilivyobinafsishwa na kutoa mapendekezo ya hatua za kuchukuliwa kwa viwanda 68 ambavyo havijaendelezwa.
“Hatua hiyo ni kuwa, tayari viwanda 14 vimerejeshwa serikalini na juhudi za kuvitafutia wawekezaji wengine walio tayari kuviendeleza zinaendelea.
Leave a comment