Friday , 19 April 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Kubenea: Amri za JPM zisivuruge utaratibu
Habari za SiasaTangulizi

Kubenea: Amri za JPM zisivuruge utaratibu

Saed Kubenea, Mbunge wa Jimbo la Ubungo akizungumza na wafanyabiashara wa Soko la Mawasiliano (hawapo pichani)
Spread the love

SAED Kubenea, Mbunge wa Jimbo la Ubungo amesema maagizo yanayodaiwa kutolewa na Rais John Magufuli kuhusu wafanyabiashara ndogo ndogo (machinga) yanasababisha migogoro kwani baadhi yao wamekuwa wakikiuka taratibu nzuri zilizowekwa na halmashauri, anaandika Hamisi Mguta.

Kubenea ameyasema hayo katika muendelezo wa ziara zake katika jimbo la Ubungo akikagua miradi ya maendeleo pamoja, kusikiliza kero za wananchi na kufanya mikutano ya hadhara inayoambata na kujibu maswali ya wananchi.

Amefanya  ziara katika hospitali ya Palestina, Soko la Mawasiliano, Soko la Sinza – A, Shule ya Msingi Mashujaa, pamoja na kuangalia hali ya barabara ya Sinza – Lion. Baadaye alimalizia na mkutano wa hadhara katika viwanja vya 7 up Sinza.

Akiwa katika soko la mawasiliano alielezwa na viongozi wa eneo hilo kuwa kumekuwa na changamoto ya baadhi ya wafanyabiashara kutokufanya shughuli zao ndani ya soko na badala yake kupanga bidhaa zao nje ya soko ambako hukwepa kulipa kodi.

“Viongozi wanasema Rais ndiyo amewaruhusu wafanyabiashara kutoka nje ya eneo la soko. Ni lazima taratibu zifuatwe, halmashauri imetumia mamilioni ya fedha kujenga soko, fedha hizo zingeweza kupelekwa hospitali, zingejenga wodi ya kina mama lakini tumeacha tukaleta huduma hapa.

“Wafanyabiashara wanapoacha kukaa hapa wakenda kukaa nje ya soko bila kulipa kodi kwa madai kuwa wameruhusiwa na rais, hizi fedha za hapa zitalipwa na nani?” amehoji.

Kubenea amesema, “Meneja wa soko ameniambia kuwa wafanyabiashara wanaopanga bidhaa nje ya stendi hii hawalipi kodi, waliopo ndani ndiyo wanalipa kodi na hao wa nje wanasema wanafuata wateja ina maana hawa wa ndani wanaolipa kodi ndiyo hawahitaji wateja?”

Katika ziara hiyo ambapo mbunge huyo alitembelea mitaa yote mitano ya Kata ya Sinza alikuwa ameambatana na wenyeviti wa mitaa husika sambamba na Godfrey Chikandamwali, diwani wa kata hiyo.

Mhasibu wa soko Mawasiliano, Imani Kisiwa akizungumza kwa niaba ya meneja wa soko amesema wafanyabiashara kutokaa ndani ya soko na kuweka vibanda barabarani ni changamoto kubwa inayoikosesha halmshauri fedha nyingi za mapato.

“Kuna meza 535 zilizokuwa zimechukuliwa na wafanyabiashara hadi sasa lakini si zote zinatumika, watu wanakimbilia nje kufuata wateja na kuacha wengine ndani wanaoshindwa kufanya biashara.

“Jambo kubwa na la kudumu ni kuwatoa wafanyabiashara wa nje ili biashara ziendelee kama kawaida kwasababu hatupokei mapato yao,” amesema.

Husna Nardo ambaye ni mfanyabiashara katika soko la Mawasilino amesema yote yaliyozungumziwa na viongozi ni ya kweli lakini utekelezaji umekuwa hafifu katika mambo yote, kuanzia kuingia kwa mabasi, na suala la wafanyabiashara kuingia ndani ya soko.

“Mimi niliyeko ndani naambiwa nilipe kodi lakini biashara haiendi kwasababu watu wengine wapo nje ya soko na waliopo nje ya soko ndio wanakua na wateja lakini hawalipi kodi. Hii si sawa,” amesema.

Akiwa katika hospitali ya Sinza – Palestina, mbunge huyo uongozi wa hospitali hiyo kupitia Dk. Krispin Kayola, Kaimu Mganga Mkuu ulielezea Changamoto wanazokabiliana nazo ikiwemo suala la miundombinu ya maji taka na upungufu wa vitanda katika wodi ya wazazi.

Kubenea aliahidi kuitatua cangamoto ya upungufu wa vitanda katika wodi hiyo na alipofika katika Shule ya Msingi Mashujaa Mwalimu Mkuu wa Shule hiyo aliomba asaidiwe kujengwa uzio wa Shule ili kuweka mazingira ya shule salama.

Alieleza kuwa wakazi kuingia maeneo ya shule kwa matumizi binafsi kama vile kujifunza kuendesha gari  na hata kutumia vyoo vya shule bila mpangilio. Kubenea alimuahidi kutoa fedha kwa shule hiyo kupitia Mfuko wa Jimbo ili uzio huo ujengwe.

Baadaye jion alihutubia wakazi wa kata ya Sinza katika mkutano wa hadhara uliofanyika viwanja vya Seven up (7 up) na kuwapa nafasi wenyeviti wa mitaa hiyo bila kujali vyama vyao, kueleza changamoto za mitaa yao.

Aidha wenyeviti hao walisifia utaratibu huo wa Mbunge kutembelea mitaa yote na kusikiliza kero za wananchi kabla ya kwenda kuwawakilisha Bungeni.

Kubenea akihutubua mkutano huo alieleza kuhusu matumizi ya fedha za mfuko wa jimbo pamoja na fedha za vijana na wanawake ambazo ni asilimia 10 ya mapato inayotolewa na halmashauri ya Ubungo.

Aliwataka vijana na wanawake kuchangamkia fursa y fedha hizo kwa kuunda vikundi vidogo vidogo ili waweze kupewa mikopo kutoka katika fedha hizo.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

KimataifaTangulizi

Mkuu wa majeshi Kenya afariki, Ruto atangaza maombolezo

Spread the loveRais wa Kenya, William Ruto ametangaza maombezo ya siku tatu...

Habari za SiasaTangulizi

Tanzania, Uturuki zanuia kukuza biashara, uwekezaji

Spread the loveSERIKALI za Tanzania na Uturuki zimekubaliana kuendeleza dhamira ya kuimarisha...

Habari za Siasa

Tume huru ya uchaguzi yatangaza ajira watendaji daftari wapiga kura

Spread the love  TUME Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), imetangaza nafasi...

Habari za SiasaTangulizi

Chadema yatangaza ruti awamu ya pili maandamano

Spread the love  CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimesema awamu ya...

error: Content is protected !!