KATIBU Mkuu wa zamani wa Umoja wa Mataifa (UN) Kofi Annan (80), amefariki dunia asubuhi leo. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Taarifa zilizopatikana mchana huu, zinaeleza kuwa Annan, aliyekuwa katibu mkuu wa saba wa umoja huo – kuanzia 1996 hadi 2006, amefariki dunia wakati akipatiwa matibabu nchini Uswisi.
Inaelezwa kuwa Annan, raia wa Ghana, aliugua ghafla – juzi usiku, na hali yake kubadilika jana na kupelekwa katika moja ya hospitali maarufu (haikutajwa) na kufariki saa 11.30 alfajiri.
Annan atakumbukwa zaidi kwa kuhuisha “heshima” ya umoja huo, baada ya kurekebisha baadhi ya miundo na kusimamia utekelezaji wa majukumu yake ipasavyo.
Mwaka 2001, alitunukiwa Tuzo ya Amani ya Nobel (akiwa mshindi sambamba na UN) kwa kile kilichoelezwa kuwa ni “kusimamia Amani ya dunia.” Tuzo za Nobel ni maarufu duniani na hutolewa kwa baadhi ya watu wanaofanya vyema na ipasavyo kusaidia “uhai” wa dunia.
Annan aliyezaliwa Mjini Kumasi, Ghana – Aprili 8, 1938 ameacha mke, Nane na watoto watatu.
Leave a comment