KUMEKUWA na hali ya sintofahamu toka kwa mashabiki na wanachama wa Yanga juu ya kiungo aliyesajiliwa msimu akitokea Mtibwa Sugar, Mohamed Banka kutoonekana uwanjani toka msimu wa Ligi Kuu ulipoanza bila maelezo yoyote kutoka kwa uongozi wa juu wa klabu hiyo. Anaripoti Kelvin Mwaipungu … (endelea).
Sababu tofauti zimekuwa zikitolewa baada ya ukimya wake wa muda mrefu huku wengine wakidai amegoma kuichezea Yanga baada ya kutomaliziwa pesa zake za usajili, huku mwenyewe alishakaliliwa akidai kuwa ni majeruhi wa goti na kubwa zaidi ni kuzuka kwa habari kuwa amefungiwa na Shirikisho la Mpira Miguu Afrika (CAF) alipokuwa katika michuano ya chalenji nchini Kenya licha ya kutojulikana ni adhabu ya muda gani.
Katibu mkuu wa klabu ya Yanga, Omary Kaya ametoa ufafanuzi juu ya mchezaji huyo kupitia kipindi cha Yanga TV, kinachorushwa hewani na kituo cha Azam TV na kusema kuwa swala la mchezaji huyo bado lipo chini ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) na kama alikuwa na adhabu yote kutoka CAF basi watapata maelekezo kutoka TFF.
“Kumekuwa na sintofahamu kuhusu mchezaji, Mohammed Banka na kweli kila mtu anazungumza analolifahamu yeye lakini pia ni wakati muhafaka kusubiri kauli husika kwa sababu hili swala lipo chini ya shirikisho na kama kuna tatizo, kufungiwa au suala la adhabu natumaini tutapata taarifa kutoka kwao na tutalizungumzia hilo jambo,” alisema Kaya.
Yanga ambayo mpaka sasa imecheza mchezo mmoja tu wa ligi dhidi ya Mtibwa Sugar katika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na kufanikiwa kuondoka na ushindi wa bao 1-0, na watu kuendelea kuipa nafasi kubwa katika kuwania ubingwa wa Ligi Kuu msimu huu.
Leave a comment