Kipima joto kilichotolewa na Kampuni ya Qwihaya General Enterprises Co Ltd kimesababisha wananchi wanaofanya kazi stendi ya Mafinga wilayani Mufindi mkoani Iringa kusimamisha shughuli zao kwa muda ili wapime joto la miili yao. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mafinga…(endelea).
Wananchi hao wakiwepo wapiga debe na wafanyabiashara ndogondogo walimteua mwenzao, akajifunza kukitumia na baadae walipanga foleni wao ili kila mmoja apime na kujua hali ya joto la mwili wake.
Kifaa hicho, tenki la kuhifadhia maji na vitakasa mikono ni miongoni mwa misaada iliyotolewa na kampuni hiyo katika mwendelezo wa kampeni yake ya kupambana na maambukizi ya ugonjwa unaosababishwa na virusi vya corona (COVID-19) katika mji wa Mafinga.
Akikabidhi msaada huo, Meneja wa Kampuni ya Qwihaya, Ntibwa Mjema amesema stendi ni kati ya maeneo yenye mikusanyiko ambayo watu wanapaswa kuwa makini kwa kufuata taratibu za afya.
Wakizungumza baada ya kupokea msaada huo, baadhi ya watu wanaofanya kazi stendi walishukuru kwa msaada huo kwa sababu hawakuwa na vifaa vya kujikinga.
“Hili tenki la maji likijaa tutatumia bila kujibana na hiki kipima joto kinaongeza hadhi ya eneo letu, ndio cha kwanza kuletwa,” amesema mmoja wa wapiga debe, Frank Kalinga.
Kwa upande wake, Ramadhani aliiomba Serikali kudhibiti mlundikano wa watu kwenye magari ya vijijini kujilinda na ugonjwa huo.
Qwihaya ni kampuni inayomilikiwa na mzalendo, Leonard Mahenda ikimiliki viwanda vya kutengeneza mbao mkoani Iringa na Kigoma.
Leave a comment