CHAMA cha Wananchi (CUF), kimeendelea kubomoka baada ya Mbaraka Chilumba, aliyekuwa Katibu Mtendaji wa Jumuiya ya Vijana wa chama hicho (JUVICUF)-Taifa kutimkia ACT-Wazalendo. Anaripoti Danson Kaijage … (endelea).
Chilumba ametangaza kujiunga na ACT-Wazalendo leo tarehe 6 Mei 2019, mbele ya wanahabari katika Makao Makuu ya chama hicho Kijitonyama, jijini Dar es Salaam.
Akizungumza mbele ya wanahabari Chilumba amesema, hata baada ya kuondoka Maalim Seif Shariff Hamad, aliyekuwa Katibu Mkuu wa CUF, bado chama hicho kimekosa mwelekeo mpaka sasa.
“Nilidhani kuondoka kwa Maalim Seif aliyedaiwa kuwa ndio tatizo, kungewezesha chama kupata mwelekeo, lakini mpaka sasa mambo ni magumu, hakuna mwelekeo,” amesema
Maalim Seif aliondoka CUF tarehe 9 Februari mwaka huu baada ya Mahakama Kuu, Kanda ya Dar es Salaam kumtambua Prof. Ibrahim Lipumba kuwa mwenyekiti halali wa chama hicho.
Maalim Seif hakuridhika uamuzi huo kwa kuwa, Prof. Lipumba aliandika barua ya kujiuzulu mwenyewe na baadaye kutaka kurejea, jambo ambalo lilisababisha chama hicho kupasuka vipande viwili.
Chilumba amesema, CUF kwa sasa haina utulivu wala dhamira ya kweli katika kuwakomboa wananchi kupitia upinzani, “nimeona hakuna mwelekeo wa kiupinzani na mimi ni mpinzani, hivyo nimeamua kuwaachia chama.”
Chilumba amekaribishwa na Sheweji Mketo, aliyekuwa mkurugenzi wa uchaguzi wa CUF ambaye naye alitimkia ACT-Wazalendo.
Chilumba anaamini kuwa, ili kuiondoa CCM madarakani, ni lazima kuwepo na muungano wa kweli na wenye nguvu kwa kuwa, chama hicho tawala kimeshindwa kukidhi matakwa ya wananchi waliokipa mamlaka.
Leave a comment