KILICHOSABABISHA kifo cha aliyekuwa Mtangazaji wa Idhaa ya Kiswahili ya Deutsche Welle (DW), Isack Gamba, ni tatizo la kuvuja damu kwenye ubongo lililotokana na presha ya damu. Anaripoti Regina Mkonde…(endelea).
Hayo yamesemwa na Mtangazaji wa Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC) Regina Mziwanda wakati akisoma wasifu wa marehemu Gamba katika ibada ya kuuaga mwili wake iliyofanyika leo tarehe 29 Oktoba 2018 katika Hospitali ya Lugalo jijini Dar es Salaam.
Regina ameeleza kuwa, kabla ya umauti kumfika Gamba hakuwahi kuugua ugonjwa wowote zaidi ya kukutwa amefariki dunia nyumbani kwake mjini Bonn nchini Ujerumani, siku ya Alhamisi tarehe 18 Oktoba 2018.
“Isaak hakuwahi kuugua ugonjwa wowote ule wa kuaminika zaidi ya kukutwa amefariki nyumbani mwake mnamo tarehe 18 oktoba 2018 siku ya Alhamisi baada ya kukosekana kazini kwa siku kadhaa, baada ya uchunguzi wa hospitali nchini Ujerumani imegundulika kwamba kilichosababisha kifo chake ni kuvuja kwadamu kwenye ubongo kutokana na presha ya damu,” amesema na kuongeza Regina.
“Shukrani, familia inatoa shukrani kwa watu binafsi na taasisi kama zifuatavyo, uongozi wa D.W kwa jitihada walizofanya kwa kufuatilia sababu za kifo na kusafirisha mwili wa marehemu kutoka Bonn hadi hapa na kuelekea Bunda, Ubalozi wa Tanzania nchini Ujerumani kwa kuhakikisha mwili unasafirishwa kurudi kwao, uongozi wa IPP Media na wafanyakazi wake, wananchi wa mkoa wa Dar es Salaam, Bunda na wote waliojaaliwa kuwa hapa.”
Kuhusu historia ya Marehemu Gamba katika enzi za uhai wake, Regina amesema hakuwahi kuoa na wala hana watoto wanaotambulika na familia yake.
Regina amesema Gamba hadi anapoteza maisha alikuwa mtangazaji wa D.W tangu mwaka 2015 akitokea Kampuni ya IPP Media katika kituo cha habari cha Redio One na ITV alikokuwa anafanyia kazi tangu mwaka 2005. Kabla ya hapo Gamba alikuwa Mtangazaji wa Redio Uhuru (2004), Redio Free Afrika (1993-1998).
Marehemu Gamba alihitimu Shahada ya Mass Communication mwaka 2010 katika Chuo cha Tumaini kilichopo jijini Dar es Salaam. A- Level alihitimu Shule ya Old Moshi (1989-1991), elimu ya sekondari alihitimu katika Shule ya Sekondari Majengo (1985-1988).
Marehemu Gamba alizaliwa tarehe 19 Januari 1970 wilayani Bunda Mjini mkoani Mara akiwa mtoto wa 12 kati ya watoto 13 katika familia yake.
Leave a comment