MWENYEKITI wa Bodi ya Wakurugenzi wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (Dawasa), Jenerali Davis Mwamunyage amesema, tatizo la maji kwa wakazi wa Kigamboni na Mkuranga litamalizika kuanzia Aprili 2021. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Mwamunyange ambaye pia ni Mkuu wa Majeshi mstaafu, amesema hayo wakati wa ziara ya kukagua maendeleo ya miradi ya maji inayotekelezwa na Dawasa katika Wilaya ya Kigamboni jijini Dar es Salaam na Mkuranga, Mkoa wa Pwani.
Amesema, anatambua hitaji la maji kwa wananchi wa maeneo hayo hivyo, mamlaka anayoisimamia inakwenda kumaliza changamoto hiyo kwa haraka ili huduma ya maji ibaki kuwa historia.
Mwamunyange amesema, kwa sasa ujenzi wa miradi hiyo inaendelea katika hatua nzuri, wakandarasi wanaendelea kwa kasi ambapo hadi kufikia Aprili 2021 hitajio la maji kwa wananchi hao litafika mwisho.
“Mradi huu wa visima vya Kimbiji na Mpera ni moja ya mradi mkubwa sana, utamaliza tatizo la maji kwa eneo la Mkuranga na Kigamboni na baadhi ya maeneo ya Temeke” amesema Mwamunyange
DAWASA inatekeleza mradi wa Maji katika Wilaya ya Mkuranga unaogharimu kiasi cha Sh. 5.5 bilioni na utahudumia wakazi takribani 25,000 huku wilaya ya Kigamboni inatekeleza mradi mkubwa wa Sh. 8.7 bilioni utakaohudumia wakazi 450,000.
Leave a comment