BARAZA la Wawakilishi nchini Marekani, limepanga kupiga kura ya Azimio la Kumdhibiti Rais wa nchi hiyo, Donald Trump, kutumia nguvu za Kijeshi dhidi ya Irani. Inaripoti Mitandao ya Kimataifa…(endelea).
Mzozo baina ya Marekani na Irani umeibuka baada ya Jenerali Qasem Soleiman, Kiongozi Mwandamizi wa Jeshi la Irani, kuuawa kwenye shambulio la anga nchini Iraqi. Shambulio lililotekelezwa kwa agizo la Rais Trump.
Nancy Perosi, Spika wa Baraza la Wawakilishi la Marekani, jana tarehe 5 Januari 2020, ameandika barua inayoeleza kwamba, baraza hilo litapiga kura juu ya Azimio la Nguvu za Vita, wiki hii. Ili kumdhibiti Rais Trump, kutotumia Jeshi kukabiliana na Irani.
Kwa mujibu wa Barua ya Perosi, Utawala wa Rais Trump ulichukua hatua ya kumuuwa Genereli Soleiman, bila kushauriana na baraza la Wawakilishi, kinyume na katiba ya Marekani.
“Kama wabunge wa Baraza la Wawakilishi, jukumu letu la kwanza ni kuwaweka salama watu na Marekani. Kwa sababu hii, tuna wasiwasi kwamba utawala ulichukua hatua hii bila kushauriana na baraza. Bila kuheshimu nguvu iliyopewa baraza na katiba,” inaeleza barua ya Spika Perosi.
Sehemu ya barua hiyo, inaeleza kwamba, hatua hiyo imelenga kumaliza uhasama wa kijeshi baina ya Marekani na Irani. Pamoja kumdhibiti Rais Trump kutumia vibaya nguvu ya jeshi.
Wakati Nancy Perosi akitangaza kuchukua hatua ya kumdhibiti Rais Trump kuanzisha vita na Irani, mamia ya watu wameandamana katika majimbo kadhaa nchini Marekani, wakipinga vitisho vya rais huyo, dhidi ya Nchi ya Irani.
Baadhi ya watu walibeba mabango yenye jumbe za kumpinga Rais Trump, na kusimama Ikulu ya Marekani ‘The White House’ na katika hoteli ya kimataifa ya rais huyo, ‘The Trump International Hotel’.
Baadhi ya mabango hayo yalieza kwamba, kodi za wananchi zitumike kwa ajili ya elimu, na si kwa ajili ya vita, huku mengine yakisisitiza ‘Hatuhitaji vita na Irani’.
Kifo cha Generali Soleiman kilichotokea Ijumaa ya tarehe 3 Januari mwaka huu mjini Baghdad nchini Iraqi, kimeleta mvutano baina ya Marekani na Iran. Ambapo mataifa hayo mawili yametambiana kufanya visasi.
Nchi ya Irani imeapa kulipiza kisasi kufuatia kifo cha Generali Soleiman, huku Rais Trump naye akitunisha mabavu, na kueleza kwamba nchi hiyo ikijaribu kuishambulia nchi yake, yuko tayari kutekekeza maeneo muhimu 52 ya Irani.
Hadi sasa Wabunge wa nchi ya Iraq, alikouliwa Generali Soleiman na Marekani, imepitisha azimio la kutaka kuondoa vikosi vya kigeni nchini humo. Kufuatia kifo hicho.
Leave a comment