MHAKAMA ya Hakimu Mkazi Mkuu, jijini Dar es Salaam imetoa ukomo wa kesi inayomkabili Halima Mdee, Mbunge wa Kawe (Chadema) ya kumtolea lugha chafu Rais John Magufuli. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Leo tarehe 26 Agosti 2019, Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba ameutaka upande wa Jamhuri kufunga ushahidi wake kabla ya Oktoba 2019.
Hakimu Simba ametoa nafasi ya mwisho kwa upande huo kuleta mashahidi waliobakia ili ufunge ushahidi wake na kisha mahakama itoe uamuzi wa kesi hiyo.
Hatua hiyo ya mahakama imekuja baada ya upande wa Jamhuri kushindwa kuleta shahidi katika kesi hiyo.
Upande wa Jamhuri leo ulishindwa kuleta shahidi na kupelekea usikilizwaji wa kesi hiyo kuahirishwa hadi tarehe 4 Septemba 2019.
Wakili upande wa Jamhuri, Sylivia Mitando amedai kwamba wameshindwa kuleta shahidi kutokana na mhusika anaumwa, na kuiomba mahakama hiyo kupanga tarehe nyingine kwa ajili ya kuendelea na ushahidi.
Kesi hiyo ilifunguliwa tarehe 10 Julai 2017, ambapo Mdee anadaiwa kutoka lugha chafu dhidi ya Rais Magufuli akiwa katika Ofisi za Chadema Kinondoni, jijini Dar es Salaam tarehe 3 Julai 2017.
Leave a comment