SERIKALI imeeleza kwamba, changamoto na kero za muungano ambazo zimetatuliwa mpaka sasa ni 11 kati ya 15 zilizowasilishwa. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Kauli hiyo ilitolewa leo tarehe 8 Aprili 2019 bungeni na Mussa Sima, Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) wakati akijibu swali la Fakharia Shomar Khamis, Mbunge wa Viti Maalum (CCM).
Katika swali lake, Fakharia alitaka kujua ni kero ngapi za muungano zimetatuliwa, na zipi ambazo hadi sasa zimeshindikana kupatiwa ufumbuzi?
Waziri Mussa amesema, changamoto nne zilizobaki zinaendelea kutafutiwa ufumbuzi na hakuna changamoto iliyoshindikana kupatiwa ufumbuzi.
Na kwamba, dhamira ya serikali zote mbili ni kumaliza changamoto zote zinazoukabili Muungano ili uendelee kudumu.
Naibu huyo amesema, hiyo ndio nguzo pekee ya kuimarisha amani, umoja na mshikamano wa chini.
Afafanua kuwa, kero nne zilizobaki na zinazofanyiwa kazi ni pamoja na mgawanyo wa mapato, uasajili wa vyombo vya moto, Tume ya pamoja na fedha na hisa za Serikali ya Mapinduzi (SMZ) na pia Bodi ya Mapato.
Amesema, moja ya majukumu ya kuimarisha Muungano ni pamoja na kuhakikisha kuwa, kero zote za zinatatuliwa.
Leave a comment