UTEUZI wa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), umefanyika huku, Prof. Mussa Assad akiwa hajui lolote. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Prof. Assad, aliyekuwa CAG kabla ya utenguzi uliofanywa na Rais John Magufuli jana tarehe 3 Novemba 2019, ametoa kauli hiyo wakati akihojiwa na Idhaa ya Kiswahili ya BBC.
Prof. Assad ameeleza kuwa, alipoteuliwa mwaka 2014 kuwa CAG alipewa barua ya uteuzi, na kwamba alitegemea angepewa barua ya utenguzi wa nafasi hiyo.
“Mimi niliteuliwa mwaka 2014, na nilipoteuliwa barua yangu ilisema kutokana na vifungu kadhaa kadhaa rais ameniteua. Sasa kwa tafsiri yangu nilitaraji barua ya kutokana na vifungu kadhaa rais ametengua uteuzi wangu.
Hilo halijafanyika sababu leo (jana) Jumapili, lakini kesho (leo) Jumatatu barua itakuja. Nitaisoma, tutaona jambo gani nilifanye. Option zote ziko available, hivyo nitajua la kufanya,” amesema Prof. Assad.
Aidha, Prof. Assad amesema kutokana na mazingira yaliyopo, alijua hilo suala ni lazima kutokea.
“Ukitazama mazingira, nilijua hiki kitu ni lazima, lakini nikasema riziki anatoa Mwenyezi Mungu na kwake haiishi. Ikiisha kazi hii ziko kazi chungu mzima za kufanya,” amesema Prof. Assad.
Leave a comment