BERNARD Membe, aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Nje, amezungumzia hatua ya kufukuzwa uanachama wa Chama cha Mapinduzi (CCM), iliyochukuliwa na Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya chama hicho, kufuatia tuhuma zilizokuwa zinamkabili za kukiuka maadili. Anaripoti Faki Sosi, Dar es Salaam … (endelea).
Kupitia ukurasa wake wa Twitter, Membe amewatoa hofu wafuasi wake, huku akiahidi kutoa taarifa kwa umma juu ya hatua hiyo, wakati wowote kuanzia sasa.
“Watanzania wenzangu nimepata habari ya kufukuzwa kwangu kutoka kwenye chama changu cha CCM. Simu zinamiminika hadi nashindwa kuzijibu. Tulieni! Nitapata muda wa kuongea na wote muda si mrefu!,” ameandika Membe saa kadhaa baada ya kufukuzwa uanachama wa CCM.
Watanzania wenzangu nimepata habari ya kufukuzwa kwangu kutoka kwenye Chama changu cha CCM. Simu zinamiminika hadi nashindwa kuzijibu. Tulieni! Nitapata muda wa kuongea na wote muda si mrefu!
— Bernard K. Membe (@BenMembe) February 28, 2020
Adhabu ya Membe ya kufukuzwa uanachama wa CCM, imetolewa leo tarehe 28 Februari 2020, na kamati hiyo baada ya kupitia taarifa ya Kamati Ndogo ya Nidhamu na Udhibiti kuhusu mahojiano juu ya tuhuma zilizokuwa zikimkabili.
Akitangaza uamauzi huo, Humphrey Polepole, Katibu wa Itikadi na Uenezi CCM, amesema Membe amefukuzwa uanachama kutokana na kushindwa kubadili muenendo wake ndani ya chama hicho tangu mwaka 2014, licha ya kupewa adhabu mara kadhaa.
“Kamati imeazimia kwa kauli moja kwamba Membe afukuzwe uanachama wa CCM, uamuzi huu umekuja baada ya kuwa taarifa zake ndani ya chama zinaonesha mwenendo wake kutoka mwaka 2014 kubadilika,” amesema Polepole na kuongeza:
“Ambako katika chama amewahi kupata adhabu nyingine ambazo zingeweza kumsaidia kujirekebisha lakini imeonekana sivyo, kwa hiyo narudia tena adhabu yake kamati imeazimia kwa kauli moja afukuzwe uanachama.”
Leave a comment