DK. Vincent Mashinji, Katibu Mkuu wa Chadema, amesema chama hakina mgogoro na aliyekuwa Mwenyekiti wa Bavicha, Patrobas Katambi ambaye ametangaza kujiunga na CCM kwa kuwa ni haki ya Kikatiba, anaandika Angel Willium.
Muda mchache baada ya Katambi kutangaza kujiunga na CCM, Dk. Mashinji, amesema: “Sisi kama chama msimamo wetu tuliuweka tangu madiwani walivyoanza kuondoka, tukaweka msimamo wazi kwamba, suala la mtu kuondoka kwenye chama au kubaki ni suala la Katiba ya nchi ambayo inampa mtu uhuru wa kuhama na kwenda kwenye chama anachotakana.”
Amesema kuwa haoni sababu ya kumzuia mtu kuondoka kwa kuwa mtu anapoamua kwenda sehemu yoyote anakuwa na matarajio.
Pia, Dk Mashinji amesema anamtakia heri (Katambi) na kuwataka CCM kumtumia katika sehemu ambavyo wanaona anafaa kutumika kwa faida ya Watanzania wote.
Hata Hivyo, Dk Mashinji amesema kuwa walikuwa wanamuandaa Katambi asaidie chama hicho kwenye kitengo cha sheria.
“Alikuwa anamalizia masomo yake ili awe wakili na tulikuwa tumeshaanza kumuandaa ili atusaidie kwenye kitengo cha sheria ndani ya chama,” amesema Mashinji.
Katambi ametangaza leo kujiunga na CCM mbele ya Mkutano wa Halmashauri Kuu ya CCM (NEC) unaofanyika katika Ukumbi wa Ikulu jijini Dar es Salaam.
Leave a comment