KATIBU Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Professa. Adolf Mkenda, amesema serikali imeanza mipango na mikakati itakayosaidia wizara hiyo kuongeza ukusanyaji wa mapato kwa kuimarisha mfumo wa kielektroniki wa usajili wa wakala wa biashara za utalii. Anaripoti Moses Mseti, Mwanza … (endelea).
Amesema kutokana na umuhimu wa sekta hiyo, tayari wizara hiyo imevitangaza vivutio vilivyopo nchini, kupitia masoko ya utalii wa kimataifa pamoja na kuupa sura mpya utambulisho wa Tanzania katika sekta ya Utalii.
Professa Mkenda ametoa kauli hiyo jijini Mwanza, wakati alipoongoza timu ya wawekezaji kutembelea Mapori ya Akiba ya Biharamuro, Burigi na Kimisi, kuangalia fursa za uwekezaji.
Alisema kuwa mipango yote inayofanyika na wizara yake inalenga kuongeza na kuchochea ukuaji wa utalii nchini kutokana Tanzania kubarikiwa vivutio vingi.
Sanjari na hayo, Professa Mkenda amesema wizara hiyo imeanza kushirikiana na Shirika la ndege Tanzania (ATCL), kuhamasisha na kuwezesha watalii wa kimataifa kutoka nchi mbalimbali kufika kwa urahisi hapa nchini.
Wizara ya Maliasili na Utalii imetangaza kwa kasi kubwa ndani na nje ya nchi fursa za uwekezaji, kwenye maeneo ya vivutio vilivyopo nchini katika kanda zote za Utalii, ikiweka mkazo zaidi kwenye Utalii wa mikutano, fukwe na meli, utalii wa kihistoria na kiutamaduni.
Leave a comment