WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola amewaonya baadhi ya watu wanaotumia ajali ya kivuko cha MV Nyerere kuichonganisha serikali na wananchi wake. Anaripoti Regina Kelvin … (endelea).
Waziri Lugola ametoa onyo hilo leo alipotembelea Kisiwani Ukerewe kushuhudia shughuli za uokoaji manusura na miili ya watu waliopoteza maisha katika ajali hiyo.
Waziri Lugola amesema kuwa, watu watakaobainika kuihusisha ajali ya MV Nyerere na tukio la kisiasa wataunganishwa na watu watakao bainika kusababisha ajali hiyo, pindi uchunguzi unaofanywa vyombo vya dola kuhusiana na ajali hiyo utakapokamilika.
“Acheni kutumia tukio hili kisiasa, waache kuchukua tukio hili kama siasa, waache kuchonganisha serikali na wananchi kwa sababu ya tukio hili, hayo ni masuala ya uchochezi, hatuko tayari kupitia tukio hili kugawa watanzania, tukiwabaini tutawakamata, na vyombo vya uchunguzi vitakapokamilika tutawaunganisha nao kwamba wao wanajua zaidi kwa hili lililotokea,” amesema.
Waziri Lugola amewataka waokoaji kuendelea na zoezi la uokoaji manusura na miili ya watu waliopoteza maisha.
Leave a comment