WIZARA ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi, imetaja kuwa ucheleweshaji wa malipo ya wakulima na wafanyakazi katika kiwanda cha chai cha Maruku mkoani Kagera ulianza Septemba, 2011 kutokana na uwezo mdogo wa kifedha wa Kagera Tea Company Ltd, anaandika Dany Tibason.
Naibu Waziri wa Wizara hiyo, William Ole Nasha alitoa kauli hiyo bungeni wakati akijibu swali la Mbunge wa Bukoba (CCM), Jasson Rweikiza.
Rweikiza alitaka kujua ni kwanini serikali haichukui hatua ya kuwasaidia wakulima na wafanyakazi ili wapate haki yao ambayo wamekuwa wakiitafuta kwa muda mrefu bila mafanikio.
“Kampuni ya chai ya Maruku imekuwa sugu kwa kutowalipa wakulima wanaoiuzia chai pamoja na kutowalipa wafanyakazi wake wenyewe,” amesema mbunge huyo.
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri amesema kutolipwa kwa wakulima na wafanyakazi hao kulitokana na uwezo mdogo wa kifedha wa Kagera Tea Ltd iliyowekwa na Spearshield Africa Company Ltd anayemiliki kiwanda cha chai cha Maruku.
Alibainisha kuwa anamiliki kwa asilimia 75 katika kusimamia uendeshaji wake ikiwemo ununuzi wa majani mabichi ya chai kutoka kwa wakulima wadogo huku wakulima hao wakimiliki asilimia 25 walizopewa na serikali kufuatia kiwanda hicho kubinafsishwa kwa Spearshield Africa Company Ltd toka kwa mamlaka ya chai Tanzania waliokuwa wanamiliki kiwanda hicho.
Alitaja sababu nyingine kuwa ni tija ndogo ya majani ya chai ikilinganishwa na gharama za uzalishaji lakini akasema serikali kupitia uongozi wa mkoa wa Kagera, Bodi ya Chai Tanzania na wakala wa wakulima wadogo wa chai Tanzania kwa nyakati tofauti walikutana na mwekezaji huyo kumwelekeza atekeleze wajibu wake wa kulipa wakulima na wafanyakazi.
Kwa mujibu wa Ole Nasha, kufuatia mikutano hiyo mwekezaji ametafuta fedha na kulipa madeni mbalimbali ikiwemo malimbikizo yote ya nyuma hadi mwezi Oktoba 2016 na ameahidi kulipa madeni ya Novemba Desemba 2016 ndani ya Januari 2017.
Leave a comment