SHIRIKA linaloshughulikia vijana na ulemavu la Raleigh Tanzania mkoani Morogoro, limewafikia watu 90 wanaoishi na ulemavu katika mikoa mitatu. Anaripoti Christina Haule, Morogoro … (endelea)
Mikoa iliyofikiwa na shirika hilo ni Dodoma, Morogoro na Iringa. Mpango wa kufikia watu hao umebebwa na kampeni ya Uwajibikaji.
Peter Lazaro, ofisa mawasiliano na mradi huo amesema, kampeni hiyo ina lengo la kuhamasisha wananchi hasa wanawake, vijana na watu wanaoishi na ulemavu kushiriki kwenye shughuli za maendeleo katika jamii zao.
Amesema, kupitia kampeni hiyo yenye kauli mbiu ‘Nawajibika,’ walengwa wanashirikisha jamii nzima kupitia vikundi kazi ambavyo vimeundwa kwa kuwajumuisha watu wenye uzoefu mbalimbali.
“Vijana ni nguvu ya Taifa hivyo wanapaswa kupewa nafasi kubwa katika kufanya maamuzi na kushiriki katika utatuzi wa changamoto mbalimbali pasipo kusubiri uongozi wa jamii yao.
“Ni kwa sababu, wao pia ni sehemu kubwa ya jamii hiyo hii itasaidia kila mwananchi katika jamii yake, kuwajibika ipasavyo na kuwa na uhuru na nguvu ya kuwaajibisha wenye mamlaka katika jamii hizo,’’ amesema Lazaro.
Pia, ofisa huyo amewaomba wadau wa maendeleo ikiwemo mashirika mbalimbali yanayotekeleza miradi ya miundombinu na huduma katika jamii, kutumia mfumo huo wa kujenga jamii yenye uadilifu ili miradi hiyo iwe endelevu.
Kampeni hiyo imepanga kufikia wananchi 538 kwa mwaka 2022, ambapo mradi huo umeanza kutekelezwa 2018 – 2022 ili wajifunze dhana ya uwajibikaji na ushirikishwaji kwa kutumia mfumo wa kujenga jamii yenye uadilifu.
Mradi huo umeandaliwa na washirika pia wadau wa maendeleo (Integrity Action) kutoka Uingereza.
Leave a comment