RAIS wa Tanzania, John Pombe Magufuli ametengua uteuzi wa viongozi watatu wa Mkoa wa Arusha na kufanya uteuzi wa viongozi watakaoshika nyadhifa hizo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea)
Taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu, Gerson Msigwa leo Ijumaa usiku tarehe 19 Juni 2020 imeelezea mabadiliko hayo.
Kwanza, Rais Magufuli ametengua uteuzi wa Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo na amemteua Idd Kimanta kuwa Mkuu wa Mkoa wa Arusha.
Kabla ya uteuzi huo, Kimanta alikuwa Mkuu wa Wilaya ya Monduli Mkoani Arusha.
Nafasi ya Mkuu wa Wilaya ya Monduli itajazwa baadaye.
Pili, Rais Magufuli ametengua uteuzi wa Mkuu wa Wilaya ya Arusha(DC), Gabriel Daqarro na amemteua, Kenan Kihongosi kuwa Mkuu wa Wilaya ya Arusha.
Kabla ya uteuzi huo, Kihongosi alikuwa Mwenyekiti wa Jumuiya ya Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) Mkoa wa Iringa.
Tatu, Rais Magufuli ametengua uteuzi wa Mkurugenzi Halmashauri ya Jiji la Arusha (DED) Dk. Maulid Madeni na amemteua Dk. John Pima kuwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Arusha.
Kabla ya uteuzi huo, Dk.Pima alikuwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kaliua Mkoani Tabora.
Aidha, Rais Magufuli amemteua, Jerry Mwaga kuwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kaliua.
Kabla ya uteuzi huo, Mwaga alikuwa Afisa katika Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI).
Wateule wote wanatakiwa kuwepo Ikulu Jijini Dar es Salaam, Jumatatu tarehe 22 Juni, 2020 saa 2:30 asubuhi.
Leave a comment