Saturday , 20 April 2024
Home Gazeti Habari za Siasa JPM awaonya wanaosaka uwaziri kwa waganga
Habari za Siasa

JPM awaonya wanaosaka uwaziri kwa waganga

Rais John Magufuli
Spread the love

RAIS wa Tanzania, John Pombe Magufuli amesema, atachelewa kuunda Baraza la Mawaziri, ili apate muda wa kuchagua mawaziri wenye sifa watakaomsaidia kutekeleza Ilani ya Uchaguzi Mkuu wa 2020/25 ya Chama Cha Mapinduzi (CCM). Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).

Kiongozi huyo wa Tanzania amesema, ameshindwa kuunda baraza hilo mapema kwa kuwa, ni kazi ngumu inayohitaji muda kwa kuwa CCM kina wabunge zaidi ya 350 wenye sifa za kuwa mawaziri.

Akizungumzia ugumu wa kuunda baraza zima la mawaziri, Rais Magufuli amesema, ugumu unatokana na mwaka huu kuwa na idadi zaidi ya 350 ya wabunge wanaotokana na Chama Cha Mapinduzi (CCM) tofauti na mwaka 2015 walikuwa wachache huku akiwaonya kutokwenda kwa waganga kutafuta nafasi hizo.

“Kazi za mawaziri na manaibu waziri hazitafika 30, sasa katika watu 350 hata ungekuwa wewe unateua ungepata shida, kwa hiyo lazima ucheki jina kwa jina kazi ni ngumu lazima uwe ‘fair’ lakini lazima umtangulize Mungu kwamba anayestahili usije ukamonea,”amesema Rais Magufuli.

Rais Magufuli amesema hayo leo Jumatatu tarehe 16 Novemba 2020 wakati anamuapisha Kassim Majaliwa kuwa Waziri Mkuu, pamoja na mawaziri wawili, Dk. Phillip Mpango (Fedha na Mipango) na Prof. Palamagamba Kabudi (Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki), Ikulu jijini Dodoma.

Majaliwa alithibitishwa na Bunge la Tanzania kuwa Waziri Mkuu baada ya kuteuliwa na Rais Magufuli tarehe 12 Novemba 2020, huku Dk. Mpango na Prof. Kabudi wakiteuliwa tarehe 13 Novemba 2020.

Uteuzi huo wa mawaziri hao umekuja siku chache baada ya John Magufuli aapishwe kuongoza Tanzania kwa mara ya pili, kufuatia ushindi alioupata kwenye Kiti cha Urais kupitia CCM katika Uchaguzi Mkuu uliofanyika tarehe 28 Oktoba 2020.

Kiongozi huyo wa Tanzania amesema“lazima nikiri sikuwa na haraka sana ya kuteua Baraza la Mawaziri na ninyi wabunge ni mashahidi kwamba mwaka huu tuna wabunge wengi zaidi ya 350 na bado wabunge wanabaki zile nafasi kumi za mimi kuteua.”

Rais Magufuli amewatoa shaka wabunge hua kuhusu uteuzi wa mawaziri akiwataka wawe na subira huku akjiwaonya wasiende kwa waganga kwa ajili ya kushinikiza kupata nafasi hizo.

“Nawaomba mnisamehe, imechukua muda mrefu, mwaka 2015 ilikuwa rahisi sababu wabunge CCM walikuwa wachache, kwa hiyo ilikuwa kazi ndogo kucheza nayo.”

“Kwa waganga nendeni shauri yenu, wengine watawapaka mikosi lakini najua hamuendi sanasana mtaenda kanisani,” amesema Rais Magufuli huku akiibua furaha kwa wageni mbalimbali waliohudhulia

Amesema, waliomba ubunge ili kuwatumikia wananchi hivyo wahakikishe wanatekeleza hilo na suala la uwaziri lisiwe kipaumbele kwao.

Rais Magufuli mara baada ya kuingia Ikulu kwa mara ya kwanza tarehe 5 Novemba 2015, alitangaza baraza lake la kwanza tarehe 10 Desemba 2015 ikiwa ni mwezi mmoja kupita.

Baadhi ya wageni waliohudhulia ni; Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan, Rais wa Zanzibar, Dk. Hussein Ali Mwinyi, Spika wa Bunge, Job Ndugai na Jaji Mkuu wa Tanzania, Profesa Ibrahim Juma.

Wengine ni; Maspika wastaafu; Pius Msekwa na Anne Makinda; Mawaziri wakuu wastaafu; John Malechela, Frederick Sumaye, Edward Lowassa na Mizengo Pinda.

Pia, Wakuu wote wa mikoa, makatibu wakuu wote wa wizara, wabunge wa Bunge la 12.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za Siasa

Dk. Mwakyembe : Zanzibar waliongoza kutaka Serikali 2 za muungano

Spread the love  MWANASIASA mkongwe nchini, Dk. Harrison Mwakyembe, amesema mjadala wa...

Habari za SiasaTangulizi

Rais Samia ataja mikakati ya kufikia trilioni 2 biashara Uturuki, Tz

Spread the loveWakati Tanzania na Uturuki zikidhamiria kuongeza kiwango cha biashara hadi...

BiasharaHabari za Siasa

Mavunde aagiza Perseus kuharakisha fidia Sengerema

Spread the loveWaziri wa Madini, Anthony Mavunde ameipongeza Kampuni ya Perseus kwa...

Habari za Siasa

Kigogo Chadema awanyooshea vidole vigogo serikalini kuhusu ripoti ya CAG

Spread the love  MWANACHAMA wa Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Boniface Jacob, amedai...

error: Content is protected !!