RAIS John Magufuli ameagiza, wageni wote watakaoingia nchini, wawekwe karantini kwa siku 14 kwa gharama zao. Anaandika Hamis Mguta,Dar es Salaam…(endelea).
kwa sasa, China inaruhusu wageni kutoka mataifa mbalimbali kuingia nchini humo kwa sharti la kuwekwa karantini kwa siku 14, ili kujiridhisha kama mgeni huyo hajaambukizwa. kwa siku zote 14, gharama ni za mgeni.
Rais Magufuli ametoa kauli hiyo leo tarehe 22 Machi 2020, alipohudhuria ibada ya Jumapili katika Kanisa la Mtakatifu Paul wa Msalaba, Jimbo Kuu la Katoliki Dodoma iliyoongozwa na paroko wa parokia hiyo Onesmo Wisi.
Pia amewataka Watanzania kutotishwa na ugonjwa huo, na badala yake waendelee kuchapa kazi na kujenga uchumi huku wakizingatia tahadhari zote za kujikinga kuambukizwa ugonjwa huo kama zilivyotolewa na Wizara ya Afya.
Katika salamu zake katika Ibada hiyo, Magufuli amesema kuwepo kwa ugonjwa wa corona isiwe sababu ya kutishana kiasi cha kumsahau Mungu.
Ametoa wito kwa Wakristo na waumini wa madhehebu mengine kumrudia Mungu ili aepusha janga hili, badala ya kumwacha shetani atawale.
Kiongozi mkuu huyo wa nchi amekemea tabia za baadhi ya watu wanaofanya mzaha juu ya ugonjwa huu ama kuwatia hofu wananchi kupitia vyombo vya habari na mitandao ya kijamii, na badala yake ametaka Watanzania waendelee kuchapa kazi huku wakizingatia tahadhari.
“Watu tusitishane, tunatishana mno. Niwaombe ndugu Wakristo na Watanzania kwa ujumla wa madhehebu yote, huu ndio wakati mzuri sana wa kumtegemea Mungu kuliko wakati wote,.”
“Tuendelee kuchapa kazi, tuendelee kuujenga uchumi wetu, hatuwezi kusalimu amri kwa ugonjwa huu wa Corona na kushindwa kumtegemea Mungu na tukashindwa kuendeleza uchumi wetu,” amesema Magufuli.
Amewashukuru viongozi wa Dini kwa kuungana na Serikali katika kuwahamasisha wananchi kuchukua tahadhari na ametoa wito kwa viongozi hao kuendelea kuliombea Taifa ili Mungu aepushe ugonjwa huo uliosababisha vifo vya watu zaidi ya 13,000 duniani kote hadi jana saa 5 usiku.
Hadi sasa rais Magufuli amesema kuna wagonjwa 12 waliothibitika kuwa na ugonjwa wa Corona lakini wanaendelea vizuri na kuwa mgonjwa wa kwanza aliyegundulika na ugonjwa huo nchini amepona.
Leave a comment