RAIS wa Tanzania, John Pombe Magufuli amefanya uteuzi wa Wakurugenzi watano wa Halmashauri (DED) nchi humo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Uteuzi wa wakurugenzi hao umetangazwa muda mdupi kupita tangu alipoteua wakurugenzi wengine watatu wa Halmashauri za mkoa wa Kilimanjaro, Mbeya na Arusha.
Taarifa iliyotolewa na Gerson Msigwa, Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu ya Tanzania imesema, uteuzi huo umeanza leo Jumamosi tarehe 4 Julai 2020.
Msigwa amesema, Rais Magufuli amemteua Duncan Golden Thebas kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Newala Mkoa wa Mtwara.
Kabla ya uteuzi huo, Thebas alikuwa Afisa Mipango wa Halmashauri ya Wilaya ya Kongwa jijini Dodoma na anachukua nafasi ya Mussa Chimae.
Pili, Rais Magufuli amemteua Mwailafu Thomas Edwin kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Mji wa Nanyamba mkoani Mtwara.
Kabla ya uteuzi huo, Edwin alikuwa Afisa Mipango wa Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi Mkoa wa Singida na anachukua nafasi ya Oscar Antony Ng’itu.
Tatu, Rais Magufuli amemteua Erica Epaphras Yegella kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mtwara Mkoa wa Mtwara.
Kabla ya uteuzi huo, Yegella alikuwa Katibu Tawala Msaidizi Mkoa wa Mbeya na anachukua nafasi ya Omari Juma Kipanga.
Nne, Rais Magufuli amemteua Hassan Njama Hassan kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero Mkoa wa Morogoro.
Kabla ya uteuzi huo, Hassan Njama Hassan alikuwa Afisa Mipango wa Halmashauri ya Mji wa Mtwara Mkoa wa Mtwara na anachukua nafasi ya Florent Kayombo.
Tano, Rais Magufuli amemteua Kanyala Malima Mahinda kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Mji wa Ifakara Mkoa wa Morogoro.
Kabla ya uteuzi huo, Kanyala Malima Mahinda alikuwa Afisa Mipango wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkuranga Mkoa wa Pwani na anachukua nafasi ya Francis Ndulane.
“Uteuzi wa viongozi hao unaanza leo tarehe 04 Julai, 2020 na wateule wote wanatakiwa kuwepo Ikulu, Chamwino Mkoani Dodoma tarehe 06 Julai, 2020 saa 4:00 asubuhi,” amesema Msigwa
Leave a comment