RAIS wa Tanzania, John Pombe Magufuli amefanya mazungumzo kwa simu na Rais wa Msumbuji, Filipe Nyusi kuhusu masuala mbalimbali yahusuyo uhusiano na ushirikiano baina ya mataifa hayo mawili ya Bara la Afrika. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Taarifa iliyotolewa leo Jumatano tarehe 1 Julai 2020 na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu, Gerson Msigwa amesema, Rais Magufuli amempongeza na kumtakia heri Rais Nyusi na wananchi wote wa Msumbiji kwa Taifa hilo kuadhimisha miaka 45 ya tangu kupata uhuru wake.
Rais Magufuli amemueleza Rais Nyusi kuwa Tanzania itaendeleza ushirikiano na uhusiano mzuri wa kidugu, kirafiki na ujirani mwema na Msumbiji kama ulivyoasisiwa na Baba wa Taifa la Tanzania, Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Hayati Samora Mosës Machel wa Msumbiji katika masuala mbalimbali yakiwemo ya kiuchumi na kijamii.
Aidha, viongozi hao wamezungumzia maandalizi ya kupokezana kijiti cha uenyekiti wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) ambapo Rais Magufuli ambaye ni Mwenyekiti wa sasa wa SADC atamkabidhi uenyekiti wa SADC, Rais Nyusi ambaye ni Makamu Mwenyekiti wa SADC kwa sasa.
Viongozi hao pia wamezungumzia ugonjwa wa homa ya mapafu inayosababishwa na virusi vya Corona (COVID-19) ambapo wamebadilishana mawazo juu ya namna bora ya kukabiliana na ugonjwa huo, hasa namna Tanzania ilivyofanikiwa kupunguza maambukizi yake.
Leave a comment