RAIS John Magufuli amesema Shirika la Ndege la Tanzania (ATCL) limekusanya mapato, kiasi cha Dola 14 milioni (sawa na TSh. 32.7 bilioni). Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Rais Magufuli amesema hayo leo tarehe 26 Oktoba 2019, katika hafla ya upokeaji ndege mpya ya serikali aina ya Boeing 787-8 Dreamliner, iliyofanyika jijini Dar es Salaam.
Rais Magufuli amesema mapato hayo yametajwa na Mhandisi Isack Kamwelwe, Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, na kuwa, atafuatilia mapato hayo kama ni kweli.
“Hizi zimenunuliwa kwa fedha za serikali hazijanunuliwa na ATCL, tumewaazima wazitumie kufanya biashara, na biashara lazima izalishe. Nilimuuliza waziri amesema wana Dola 14 miliono, nitakwenda kuzicheki kesho kwenye akaunti,” amesema Rais Magufuli.
Rais Magufuli ameuagiza uongozi wa ATCL kutekeleza majukumu yao vizuri, ili shirika hilo lijiendeshe kwa faida.
“Nitoe wito, kwanza kwa management (uongozi) na watumishi wa ATCL, tekelezeni majukumu yenu vizuri,” amesema Rais Magufuli.
Leave a comment